Saturday, November 18, 2017

DED HALMASHAURI MJI WA MBINGA "AJISAFISHA" KWA MADIWANI WAKE

Madiwani wa Halmashauri mji wa Mbinga wakivaa majoho kabla ya kuanza kikao chao cha baraza la Madiwani kujadili taarifa za maendeleo ya wananchi robo ya kwanza ya mwaka kilichofanyika juzi kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi mjini hapa.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Robert Kadaso Mageni amezungumza katika baraza la Madiwani wa halmashauri ya mji huo akieleza kwamba matatizo yaliyojitokeza nyuma kati yake na Madiwani hao hakuna ubaya wowote na kazi zinaendelea kufanyika.

Mageni alisema hayo juzi mbele ya msaidizi wa Katibu tawala wa mkoa huo, Joel Mbewa katika kikao cha Madiwani kilichoketi kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi mjini hapa.

Madiwani hao walipozungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wetu walisema kuwa kufuatia mgogoro mzito unaoendelea kufukuta kati yake na Madiwani wa mji huo, juu ya uvunaji wa msitu wa Mbambi ambao anashutumiwa kwamba yeye na baadhi ya watendaji wake wametafuna kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 800 ndiyo maneno hayo sasa amekuwa akiyazungumza kwa lengo la kutaka kujisafisha.

Walisema kauli hiyo ya Mkurugenzi huyo inafuatia pia Madiwani hao katika kikao walichoketi Oktoba 27 mwaka huu kumkataa hawataki kufanya naye kazi tena.

Vilevile sakata hilo la kumkataa liliwafanya wasipokee agenda za kikao na hatimaye wote walitoka nje ya kikao na kuacha kuendelea nacho ndipo juzi Novemba 14 mwaka huu, baada ya taratibu husika kufanyika na kupitia vikao mbalimbali wameweza Madiwani hao kukutana kwa pamoja na kujadili tena agenda za maendeleo ya wananchi na sio mgogoro wa msitu huo ambao unasubiri maamuzi yake baada ya kufikishwa ngazi za juu Serikalini.

Pamoja na mambo mengine, Mageni alionekana kutumia muda wake kwa mtindo wa “kujisafisa” akisema yeye anatambua kwamba baraza hilo la Madiwani wanapaswa kusafiri meli moja katika wajibu wa kutekeleza miradi ya maendeleo ya wananchi.

“Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yaliyotokea matokeo yapatikane suala la mtikisiko wa pamoja lakini safari yetu ni lazima tuwatumikie wananchi, kama mnavyofahamu Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli ametuamini tutekeleze maendeleo ya wananchi,

“Hakuna ubaya wowote kazi tunaendelea kufanya kama tulivyokuwa tunafanya kuhakikisha Serikali yetu tunafikisha lengo katika kusukuma mbele maendeleo”, alisema Mageni.

Kadhalika alimuomba Mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Mbinga, Kipwele Ndunguru pamoja na Madiwani wake waendelee kushirikiana kutekeleza maendeleo ya wananchi.

Awali akizungumza katika baraza hilo, msaidizi wa Katibu tawala wa mkoa wa Ruvuma, Joel Mbewa alisema kuwa kuanzia sasa viongozi wa kutoka ngazi ya mkoa Ofisi ya Katibu tawala watakuwa wanahudhuria kikao hicho cha baraza la Madiwani kila kitapokuwa kinafanyika.

“Madiwani niwasisitize mnapokuwa kwenye vikao vyenu vya CMT muwe mnajenga hoja na misimamo yenu huko kwa kutoa mawazo yenu na matatizo yaliyopo kwenye kata ili yaweze kufanyiwa kazi”, alisema Mbewa.

Pia amewataka washirikiane na Mkaguzi wa ndani pamoja na Mwanasheria wa halmashauri katika kusimamia miradi mbalimbali ambayo inatekelezwa ndani ya halmashauri.

“Mwanasheria na Mkaguzi wa ndani haya ndiyo macho mawili ndani ya halmashauri yenu ambayo yanatusaidia katika kuona mbali zaidi tushirikiane nao kutatua matatizo”, alisisitiza.

Mbewa alieleza kuwa halmashauri pia inatakiwa kuongeza juhudi katika ukusanyaji wa mapato ili utekelezaji wa miradi ya wananchi uweze kufanyika ipasavyo.

No comments: