Sunday, November 19, 2017

KAYOMBO AMWAGIWA SIFA MCHANGO WAKE WA KUKUZA SEKTA YA ELIMU MBINGA

Viongozi mbalimbali wa wilaya ya Mbinga wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Ubalozi wa Korea kusini akiwemo na aliyekuwa Mbunge wa Mbinga, Gaudence Kayombo (Aliyeketi akiwa amevaa suti rangi nyeusi kutoka upande wa kulia) siku ya uzinduzi wa eneo la ujenzi wa Kituo cha elimu, Novemba 15 mwaka huu katika eneo la mtaa wa Lulambo kata ya Matarawe mjini hapa.  
Na Kassian Nyandindi,   
Mbinga.

PONGEZI zimetolewa na baadhi ya Wananchi wanaoishi katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, kwa jitihada za kuchangia maendeleo katika mji huo zinazofanywa na aliyekuwa Mbunge wao, Gaudence Kayombo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari hizi wananchi hao walisema kuwa Kayombo, wanampongeza kwa kutafuta Wafadhili kutoka Ubalozi wa Korea kusini na hivi sasa wanatarajia kuanza kujenga Kituo cha elimu katika mtaa wa Lulambo kata ya Matarawe mjini hapa.

“Ushirikiano huu anaoufanya wa kutujali na kutukumbuka sisi wananchi wake ni ishara tosha inayothibitisha ni mtu ambaye anafaa katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo yetu, tunachoomba kituo hiki kijengwe kwa wakati ili kuweza kuanza kutoa huduma kwa jamii”, walisema.

Vilevile walieleza kuwa umefika wakati sasa mji wa Mbinga unapaswa kuwa na maendeleo yanayokua kwa kasi, hususan katika sekta ya elimu ambayo ndiyo msingi mkuu wa kukuza vipaji vya aina mbalimbali kwa vijana na faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Awali akizungumza katika sherehe za uzinduzi wa eneo la ujenzi wa kituo hicho zilizofanyika Novemba 15 mwaka huu kwenye kata hiyo Mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Mbinga, Kipwele Ndunguru alipongeza hatua hiyo na kueleza kuwa ujenzi huo unapaswa kuungwa mkono kwa asilimia kubwa ili mji huo uweze kuwa na maendeleo.

“Tukio hili ni la kimaendeleo tunajua Mbinga tumekwama katika shughuli nyingi sana za maendeleo ujenzi wa chuo hiki utazalisha mafunzo mengi ya ualimu na sekta ya afya”, alisema Ndunguru.

Pamoja na mambo mengine, kukamilika kwa ujenzi wa kituo hicho ambacho ni chuo cha mafunzo katika sekta ya elimu na afya utagharimu dola za Kimarekani milioni 150.

No comments: