Sunday, November 5, 2017

MAKALA: YA MAGENI MBINGA MSITU WA MBAMBI FUNDISHO KWA VIONGOZI WENGINE WAHUSIKA WAWAJIBISHWE

Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga hivi karibuni wakitoka nje ya kikao baada ya kumkataa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Robert Kadaso Mageni ambapo kikao cha baraza la madiwani hao kilivunjika wakikataa kuendelea kufanya kazi na mkurugenzi huyo na mpaka sasa haijulikani hatma ya sakata hilo.
Na Dustan Ndunguru,

DOKTA John Pombe Magufuli ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tangu aingie madarakani mwaka 2015 amekuwa akiwaasa Watanzania kuwa wazalendo kwa nchi yao ambapo hata wateule wake amewataka kufuata nyendo za serikali yake anayo iongoza, ili kwa pamoja waweze kuleta mabadiliko ya kweli ambayo wananchi wamekuwa wakiyalilia.

Ni ukweli usiopingika kwamba Rais Magufuli siku zote amekuwa akipambana na mafisadi ambao miaka mingi wamekuwa na kawaida ya kuiba rasilimali za Watanzania, jambo ambalo linawafanya wananchi walio wengi wakumbwe na changamoto nyingi ikiwemo ubovu wa barabara, ukosefu wa madawa kwenye zahanati na hospitali na mengine mengi huku wale ambao waliamua kwa makusudi kujilimbikizia mali wakiishi kama wafalme bila kuwajali wengine wenye shida.

Serikali ya awamu ya tano imeonesha dhamira ya dhati katika kuwatumikia wananchi wake ikiwemo kusimamia kikamilifu rasilimali zilizopo kama vile madini.


Hali hiyo imewafanya wananchi kujenga imani kwa Serikali yao waliyoichagua ukizingatia kwamba, matunda ambayo wamekuwa wakiyakosa kwa miaka mingi wameanza kuyaona kwa njia mbalimbali.

Lakini yatupasa kutambua kuwa Rais Magufuli siku zote hapendi na amekuwa akichukizwa kuona pale mteule wake akikiuka maagizo aliyopewa ambayo amekuwa akiyatoa kila mara hasa katika kusimamia rasilimali za taifa hili ambazo kama inavyofahamika, wakati mwingine zimekuwa zikitumika vibaya na baadhi ya watu wachache ambao wamekuwa na tabia mbaya ya kutaka kujilimbikizia mali za wananchi na hatimaye mwisho wa siku anemeeke yeye binafsi huku mwananchi wa kawaida akiendelea kubaki kuwa maskini.

Ikumbukwe kuwa wakati Wakurugenzi wa halmashauri za miji, manispaa, majiji na wilaya wanaapishwa walisisitizwa kusimamia mapato ya ndani katika halmashauri zao ili waweze kutekeleza miradi ya maendeleo na kuwahudumia wananchi ipasavyo.

Pamoja na kuapishwa, Wakurugenzi hao walikula kiapo cha maadili ya utumishi wa umma pamoja na ahadi ya kuwa waaminifu na wazalendo kwa nchi yao ambapo baada ya hapo kila mmoja wao alikwenda kwenye eneo lake la kazi tayari kutekeleza majukumu yake ya kazi aliyopewa.

Wakurugenzi hawa wanaowajibu wa kusimamia mikataba iliyopo na ile ambayo halmashauri inaingia na Wazabuni walioshinda tenda mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuzingatia masharti ya mikataba hiyo wakati wa utekelezaji wake huku wakitakiwa kuwa wazi katika uwajibikaji wake kwa mamlaka husika waliyonayo kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Binafsi natambua kuwa Mkurugenzi mtendaji katika halmashauri yoyote ile ndiye anayebeba bendera ya maendeleo na dhamana ya kusimamia sekta zote ndani ya halmashauri ikiwemo afya, kilimo, elimu, maji, uvuvi ambazo zikisimamiwa vizuri huwaletea maisha bora Watanzania.

Haya yote yanawezekana endapo tu mteule huyo wa Rais atakuwa makini kutekeleza majukumu yake ya kazi aliyopewa, ikiwemo kutembelea maeneo yake katika halmashauri na kujionea changamoto zinazowakabili wananchi wake ikiwemo kuzitafutia ufumbuzi wa haraka badala ya kukaa muda mwingi ofisini.

Kana kwamba haitoshi Mkurugenzi huyo anaowajibu wa kufuatilia na kusimamia miradi ya maendeleo iliyopo ndani ya halmashauri yake kwa kuzingatia matumizi sahihi ya fedha zilizotolewa na Serikali ili kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Robert Kadaso Mageni.
Oktoba 20 mwaka huu kwa mujibu wa kumbukumbu zilizopo kilifanyika kikao maalum cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, ambapo Wajumbe wa Kamati maalum ya kuchunguza ubadhirifu wa fedha za msitu wa Mbambi unaomilikiwa na mji huo siku hiyo ya kikao walikuwa wakiwasilisha taarifa za uvunaji wa msitu huo ambao kazi hiyo ya uvunaji ilifanyika mapema kuanzia mwezi Januari mwaka huu.

Baada ya taarifa ya kamati kutolewa ilionesha wazi kuwa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya mji huo, Robert Kadaso Mageni alikuwa mmoja kati ya watendaji ambao walishiriki katika kuhujumu mapato ya msitu huo na hivyo kuingiza hasara ndani ya halmashauri jambo ambalo mpaka sasa limeweza kuzua gumzo kubwa na kuwakatisha tamaa wananchi wa kata ya Matarawe na maeneo mengine kuzunguka halmashauri hiyo ambao kwa miaka 30 wamefanya kazi kubwa ya kushiriki katika kuutunza msitu huo.

Katika taarifa iliyosomwa na Katibu wa kamati hiyo maalum iliyoundwa na baraza hilo la Madiwani Julai 27 mwaka huu, limetoa mapendekezo yake ya kumkataa Mkurugenzi huyo kwamba hawataki kufanya naye kazi tena, wakimtuhumu ametafuna fedha za mauzo ya mbao zilizopasuliwa katika msitu wa Mbambi uliopo mjini hapa ambao ni mali ya halmashauri ya mji huo.

Imeelezwa kuwa Mageni anaingia katika kashfa pia ya kulipotosha baraza hilo katika kikao walichoketi mwezi Novemba 2 hadi 3 mwaka jana na kutoa taarifa za uongo kwamba msitu huo una jumla ya miti 5,4040 ambayo inafaa kupasuliwa mbao wakati ukweli ni kwamba msitu ulikuwa na miti 8,470.

Kufuatia taarifa hizo ambazo hazikuwa sahihi wakati anazitoa kwenye baraza hilo juu ya uvunaji wa msitu huo, hali hiyo imesababisha halmashauri kupata hasara ya zaidi ya shilingi milioni 800 wakati huo huku halmashauri anayoiongoza ikiendelea kukabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinalenga mahitaji ya wananchi ikiwemo hospitali ya wilaya hiyo kukosa hata gari la kubebea wagonjwa, majokofu ya kuhifadhia maiti pamoja na chumba bora cha kufanyia upasuaji.

Baada ya baraza hilo kutoa mapendekezo hayo ya kumkataa, walimtaka Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye kufikisha kilio chao kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli ili aweze kuchukua hatua zaidi za kinidhamu dhidi ya mtumishi huyo.

Akiwasilisha taarifa ya uchunguzi wa tuhuma hizo mbele ya baraza hilo ambalo lilihudhuriwa na mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga wakiwemo na Wajumbe wa kamati yake ya ulinzi na usalama, katibu wa kamati ya kuchunguza tuhuma hizo Benedict Ngwenya ambaye ni diwani wa kata ya Mpepai alisema kuwa Mkurugenzi, Mageni ameshirikiana na watendaji wake wa halmashauri ya mji huo kuhujumu mapato hayo.

Ngwenya anafafanua kuwa ufisadi huo uliofanyika, Mkurugenzi ameshirikiana na baadhi ya watendaji wake wa halmashauri ambao waliteuliwa kwa ajili ya kufanya kazi ya kusimamia uvunaji wa msitu wa Mbambi ambao watendaji hao aliwataja kuwa ni Afisa misitu wa halmashauri ya mji huo, David Hyera na mlinzi mkuu Efreim Kawonga.

“Kwa msingi huu kamati ilibaini mbao nyingi ziliibwa kwa kisingizio kwamba zimekwenda kwenye shughuli ya mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa wakati sio kweli na hata fedha zilizotokana na uvunaji huo tumefuatilia kwenye akaunti husika hakuna fedha iliyoingizwa”, alisema Ngwenya.

Anafafanua kuwa thamani hiyo halisi na ubadhirifu uliofanyika katika msitu wa Mbambi waliweza kuipata baada ya kamati hiyo kufanya uchunguzi wa kina kwa kuwatumia wataalamu waliobobea katika masuala ya uvunaji wa misitu ambao walitoka nje ya halmashauri ya mji wa Mbinga.

“Mapendekezo ya awali aliyoyaleta Mkurugenzi huyu Novemba 12 mwaka 2016 katika baraza lililopita la Madiwani alituambia kwamba msitu huu baada ya mavuno zingepatikana shilingi milioni 325,000,000 lakini hadi leo hii tunaambiwa mapato yaliyopatikana ni shilingi milioni 130,000,000 tu jamani kweli hata katika mtazamo wa kawaida jambo hili linaweza kuingia akilini ?”, alihoji Ngwenya.

Anaeleza kuwa hasara hiyo iliyopata halmashauri kutokana na uzembe uliofanyika na watendaji hao ambao wamepewa dhamana na Serikali kusimamia shughuli za maendeleo na mali za umma, wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufukuzwa kazi ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Ngwenya anaongeza kuwa hasara hiyo imesababishwa pia kutokana na taratibu husika zilizowekwa wakati wa kupasua mbao katika msitu huo, hazikufuatwa kwa mujibu wa sheria za nchi ikiwemo kwamba hata Mkurugenzi huyo amekiuka baadhi ya sheria ambazo zinakataza suala la Serikali kufanya biashara ya kuuza mbao badala yake ilitakiwa kuuza miti iliyopo kwenye msitu huo baada ya upembuzi yakinifu kufanyika.

Anabainisha kwamba Mkurugenzi, Mageni alipaswa pia kulieleza bayana baraza hilo la Madiwani kwamba Serikali haifanyi biashara ya mbao kwa mujibu wa sheria hiyo lakini alilipotosha na hakuweza kutoa ufafanua wowote ikidaiwa kuwa alikuwa na lengo la kutaka kujinufaisha yeye binafsi kupitia mauzo ya mbao hizo.

“Kama tungefuata taratibu za Serikali hasara hii tungeweza kukabiliana nayo lakini mtaalamu wa misitu, Hyera alishindwa hata kumshauri Mkurugenzi wake juu ya taratibu za zabuni za uvunaji wa msitu huu, badala yake wametumia mbinu za ujanja kumtafuta mzabuni ambaye wanamjua wao bila kufuata taratibu husika ambapo kamati hii maalum ilipofanya uchunguzi wa kina tumebaini zabuni ya kuvuna msitu ule na mikataba yake haikufuata taratibu”, anasema.

Naye Mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Mbinga, Ndunguru Kipwele akizungumza katika kikao hicho anasema kuwa anaipongeza kamati kwa kazi nzuri iliyofanya ya kuchunguza jambo hilo na kueleza kuwa baraza linaafiki juu ya mapendekezo yaliyotolewa kwa kuiomba Serikali ichukue hatua kali za kinidhamu dhidi ya Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo kwa kuwa mamlaka iliyomteua ni ya Rais wa nchi.

Kadhalika alisema baraza limependekeza pia mtaalamu wake wa misitu, Hyera na mlinzi mkuu, Kawonga wafukuzwe kazi na kufikishwa kwenye vyombo vya kisheria.

“Niwaombe watendaji wetu kwa dhati wote kwa pamoja tumsaidie Rais wetu maana ana dhamira nzuri sana kwa watanzania lakini inakuwa pia nia aibu kwa mteule wake kutenda hayo ambayo yamefanyika na kuikosesha halmashauri mapato yake”, anasema Kipwele.

Alipohojiwa na waandishi wa habari, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Mageni anasema kuwa yeye hawezi kuzungumzia jambo lolote hivi sasa juu ya tuhuma hizo kama ni za kweli au la.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Nshenye aliipongeza kamati hiyo ya uchunguzi wa msitu wa Mbambi huku akieleza kuwa, “taarifa hii waliyoitoa hapa ni ya kweli kabisa kwa hiyo mimi niwapongeze sana na sisi kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya baada ya kutoka hapa tunayo ya kufanya”, anasema Nshenye.

Kwa upande wake Hamis Nanyanje ambaye ni mkazi wa kata ya Matarawe ambaye pia alihudhuria kikao hicho cha baraza la madiwani pamoja na kutoa pongezi kwa madiwani hao alisema akiwa mwananchi wa kata hiyo hakutegemea kama bado kuna baadhi ya watumishi hapa nchini, ambao hawana uzalendo wa kweli na wanaendekeza vitendo vya kutumia mali za umma kwa manufaa yao binafsi.

Nanyanje anaeleza kuwa jambo pekee lililopo hivi sasa ni kwa wananchi na viongozi kushirikiana kuendelea kuwaumbua wale wote ambao wataonekana kwenda kinyume na maagizo yanayotolewa na Rais Magufuli ya kuwataka Watanzania kutanguliza uzalendo kwa nchi yao na sio vinginevyo.

Naye Emmanuel  Mapunda mkazi wa Mbinga mjini anasema kwa hayo yaliyotokea katika msitu wa Mbambi ni ushahidi tosha kuwa bado wapo watendaji wachache katika halmashauri, ambao wanamawazo ya kutumia vibaya mali za umma kwa kujinufaisha wao binafsi huku wananchi wakiendelea kuumia kwa kukosa huduma muhimu ambazo walipaswa kuzipata kutokana na mapato yao ya ndani.

Kwa msingi huo hayo ambayo yamejitokeza katika halmashauri ya mji wa Mbinga ya kuvuna msitu ambao wananchi wamekuwa wadau wazuri kwa kipindi cha miaka 30 kuutunza, na kwamba baada ya uvunaji wamejitokeza watu wachache kutumia vibaya madaraka yao kwa kuhujumu mapato ya msitu huo ni wakati sasa hatua stahiki dhidi yao zichukuliwe ili iweze kuwa fundisho kwa viongozi wengine na sio vinginevyo.

Ni dhahiri kuwa mapato ya msitu huo yangeweza kusaidia kuwaondolea adha wananchi wa wilaya hiyo na majirani zao kwa kununua gari la kubebea wagonjwa na kutatua kero nyingine.

Kutokana na matumizi haya mabaya ya fedha hizo tayari ile asilimia 10 ambayo hata wananchi walipaswa kupewa kupitia vikundi vya vijana na wanawake sote tunatambua imepotea, ambao makundi hayo yataendelea kuumia kwa kukosa fedha ambazo zingeweza kuwasaidia kuanzisha miradi mbalimbali ya ujasiriamali.

Sasa Madiwani wa halmashauri ya mji wa Mbinga mnapaswa kuendelea kusimamia na kufuatilia kikamilifu hata fedha zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maendeleo ndani ya halmashauri yenu, ili kuweza kuona kama kweli zinafanya kazi ile ambayo imepangwa na kwa viwango vinavyokubalika.

Hata hivyo nashauri kuwa tunapobaini kuna ubadhirifu au matumizi yasiyo sahihi ya fedha hizo, wasisite kuchukua hatua stahiki kama walivyofanya kwenye msitu huu wa Mbambi uliopo katika kata ya Matarawe halmashauri ya mji huo.

No comments: