Thursday, November 16, 2017

WAUMINI ANGLIKANA SONGEA WACHANGA MAMILIONI YA FEDHA KUJENGA KANISA

Na Albano Midelo,    Songea

WAUMINI wa Kanisa la Anglikana la Mtakatifu Augustino Mjimwema Songea Dayosisi ya Ruvuma, wamechanga zaidi ya shilingi milioni 57 kwa ajili ya ujenzi wa kanisa hilo.

Katibu wa kanisa hilo Dokta Daniel Mtamakaya alisema ili waweze kukamilisha ujenzi wa kanisa hilo, zinahitajika zaidi ya shilingi milioni 186.

Dokta Mtamakaya alisema kuwa kanisa hilo limefanikiwa pia kuchangisha zaidi ya shilingi milioni 33 ambazo zitatumika kwa ajili ya kuezeka kanisa na kwamba kinachohitajika hivi sasa ni shilingi milioni 15 ambazo ni gharama za kumlipa fundi.

Kwa mujibu wa Katibu huyo aliongeza kuwa wameweza kujenga shule ya Jumapili (Sunday School) ambayo ujenzi wake utagharimu zaidi ya milioni tano hadi utakapokamilika miundombinu yake.

“Mara tu baada ya kuezeka kanisa jipya, kanisa dogo linalotumika hivi sasa, litabadilishwa matumizi ili iweze kuwa nyumba ya kuishi wahudumu wa kanisa na kuweza kuepuka kuwalipia pango ambalo hugharimu fedha nyingi kanisa”, alisema.

Akizungumza baada ya kupata taarifa ya ujenzi wa kanisa hilo, Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Ruvuma Mhashamu Raphael Haulle aliwapongeza waumini wake kwa kugharamia ujenzi huo na kuanzisha shule ya watoto.

Askofu Haulle alieleza kuwa kanisa linaendelea kufanya jitihada ya kutafuta wafadhili wa ndani na nje ya nchi ili kuharakisha ujenzi huo ambao asilimia kubwa zimetumika nguvu za waumini wenyewe.

“Najaribu kuwasiliana na wafadhili wa ndani na nje ya nchi, baadhi ya wafadhili toka nchini Ujerumani wamefika hapa kuangalia kanisa hili, naamini Mungu atatupa fedha za kuezeka na kukamilisha ujenzi wa kanisa hili’’, alisema Askofu Haulle.

Vilevile alitoa wito kwa watu wote wenye mapenzi mema kutoka ndani na nje ya nchi kutoa mchango wowote ili kuweza kukamilisha ujenzi wa kanisa hilo.

No comments: