Tuesday, November 14, 2017

VIONGOZI WATAKIWA KUSIMAMIA BEI YA PEMBEJEO ZA KILIMO

Na Mwandishi wetu,  
Songea.

MKUU wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma Palolet Mgema amewataka viongozi wa ngazi mbalimbali wilayani humo, kusimamia ipasavyo bei ya pembejeo za kilimo ili kuepusha ulaghai unaoweza kufanywa na baadhi ya mawakala ambao sio waaminifu waliopewa dhamana na Serikali kusambaza pembejeo hizo kwa wakulima katika kuelekea msimu huu wa kilimo.
Palolet Mgema.

Mgema alitoa agizo hilo mwishoni mwa wiki alipokuwa akitoa salamu za Serikali kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Madaba huku akisisitiza kuwa wanaowajibu pia wa kusimamia hilo kuhakikisha mkulima anauziwa kwa bei iliyopangwa.

Alisisitiza kuwa endapo viongozi hao watapuuza na kuwaachia mawakala wafanye wanavyotaka, kuna uwezekano mkubwa kwa wakulima kuuziwa kwa gharama kubwa hatimaye kushindwa kumudu gharama husika na kusababisha baadhi yao kutozalisha mazao yao shambani.

Katika hatua nyingine, Mgema alisema kuwa Ng’ombe ambao wamezuiliwa kuingia katika wilaya ya Songea wanaotoka maeneo mengine nje ya wilaya hiyo, ni wale wanaoingizwa kwa ajili ya kutafuta malisho na ufugaji hivyo Serikali imeruhusu kuingizwa kwa ng’ombe wanaoletwa kwa ajili ya wananchi kupata nyama tu na sio vinginevyo.

Alisema tatizo kubwa la uingizaji wa mifugo kiholela katika wilaya ya Songea hasa kwa halmashauri ya wilaya ya Madaba limechangia kwa kiasi kikubwa baadhi ya watumishi waliopo kwenye halmashauri hizo ambao wamepewa dhamana ya kusimamia hilo kujihusisha na vitendo vya rushwa huku baadhi yao wakiruhusu wafugaji kuingiza mifugo yao bila kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.

Hata hivyo aliwataka viongozi hao watekeleze maagizo wanayopewa na Serikali ipasavyo na sio kuyapuuza kwani atakayefanya tofauti kinyume na taratibu zilizowekwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

No comments: