Monday, November 20, 2017

WATU 72 WANAOISHI KIPIKA MBINGA WANUSURIKA KUPOTEZA MAISHA WAKIDAIWA KUNYWA KINYWAJI CHENYE SUMU


Wagonjwa wanaodaiwa kunywa kinywaji aina ya togwa kinachodaiwa kuwa na sumu wakiwa wamelazwa katika hospitali ya Mji wa Mbinga.

Baadhi ya Wahudumu wa afya katika hospitali ya Mji wa Mbinga wakiendelea kuwahudumia wagonjwa jana ambao wanadaiwa kunywa kinywaji kinachodaiwa kuwa sumu aina ya togwa, ambacho hata hivyo hali za wagonjwa hao zinaendelea vizuri baada ya kuwahi matibabu katika hospitali hiyo.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WATU 72 ambao ni Wakazi wa kitongoji cha Kipika kata ya Matarawe katika Mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wamenusurika kupoteza maisha baada ya kunywa kinywaji aina ya togwa kinachodaiwa kuwa na sumu.

Aidha imeelezwa kuwa tukio hilo lilitokea Novemba 19 mwaka huu majira ya mchana, ambapo kinywaji hicho walikunywa wakiwa kwenye sherehe (Harusi) iliyokuwa ikifanyika katika kitongoji hicho.

Mmoja kati ya wagonjwa waliolazwa katika wodi ya wanaume hospitalini hapo, Chirwa Mohamed Hassan akizungumza na mwandishi wetu alisema kuwa baada ya kunywa kinywaji hicho na masaa machache kupita, ghafla yeye na wenzake walijikuta tumbo linauma na kuanza kuharisha mfululizo ndipo walikimbizwa hospitali kwa matibabu zaidi.

“Baada ya kula chakula tulipewa togwa tulikuwa tunakunywa masaa machache yalipopita ndipo tumbo lilianza kuuma na kuharisha lakini baada ya kuwahi hapa hospitalini, tunawashukuru waganga kwa kutupatia matibabu kwa uharaka na sasa tunajisikia kuna unafuu kidogo”, alisema Hassan.


Naye Cecilia Venant Ndomba ambaye amelazwa katika wodi ya wanawake alifafanua kuwa yeye alipomaliza kunywa togwa hiyo tumbo lake lilianza kuuma na kuanza kutapika ghafla.

“Kufikia majira ya saa kumi jioni hapa hospitalini wakati tunaletwa tulikuwa hatujuani mimi nilipoteza fahamu tumbo langu lilikuwa linanyonga sana”, alisema Ndomba.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa hospitali ya Mji wa Mbinga, Festo Mapunda alithibitisha kuwapokea wagonjwa hao na kueleza kuwa mpaka sasa yeye na timu yake ya wataalamu wa hospitali hiyo inaendelea kufanya uchunguzi, ili waweze kubaini chakula na vinywaji walivyokula kama vilikuwa na sumu au la na taarifa zitatolewa tena baadaye.

“Wagonjwa walioripotiwa mpaka sasa ni 72 tunaendelea kuchukua sampo ya vyakula katika eneo lile la sherehe ili tuweze kufanya utafiti wa kina, lakini tumebaini mpaka sasa hawa wagonjwa wamekula uchafu ambao ulikuwa kwenye chakula”, alisema Mapunda.

Mapunda alisema kuwa kati ya wagonjwa hao waliolazwa katika hospitali hiyo 46 ni wanawake, 23 ni wanaume na watatu ambao ni wanaume pia walipatiwa matibabu na kuruhusiwa kurudi nyumbani.

No comments: