Saturday, November 25, 2017

MAJALIWA ASIKITISHWA NAMTUMBO KUWA NA REKODI MBAYA WANAFUNZI KUPATA UJAUZITO

Na Kassian Nyandindi,  
Namtumbo.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali ya awamu ya tano itaendelea kuweka miundombinu ya uhakika katika sekta ya elimu hapa nchini, ili kuweza kutoa fursa kwa watoto waliopo shuleni waweze kusoma vizuri na kutimiza malengo yao ya maendeleo ya maisha ipasavyo.

Majaliwa alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na wanafunzi wa shule ya Sekondari Nasuli wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma huku akiwataka wazazi watekeleze jukumu la kila mtoto mwenye umri wa kwenda shule ni lazima apelekwe shuleni ili aweze kusoma.

Aidha alifafanua kuwa mpango wa Serikali hivi sasa ni  kuhakikisha kwamba kila kwenye shule ya kidato cha kwanza hadi cha nne kunakuwa na shule ya kidato cha tano, ikiwa ni lengo la kuwarahisishia watoto wanaofanya vizuri katika mitihani yao ya kumaliza kidato cha nne waendelee na  masomo yao jambo ambalo litasaidia kupata vijana wengi watakaokwenda vyuo vikuu.


Kwa mujibu wa Waziri mkuu alieleza kuwa katika mkakati huo Serikali imetoa nafasi kwa watu binafsi na mashirika mbalimbali kuanzisha vyuo vikuu ili watoto wengi zaidi wajiunge na vyuo hivyo na hatimaye Taifa liweze kupata wasomi wengi zaidi watakaotumikia nchi yetu.

Alisema kuwa katika kufanikisha malengo hayo wametenga zaidi ya shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kununua seti za masomo na tayari zimeshaanza kusambazwa katika shule mbalimbali hapa nchini ili kuwarahisishia watoto kuwa na uelewa mkubwa katika masomo yao.

Hali kadhalika Majaliwa amewataka watoto kuwa wavumilivu wakati huu ambao Serikali inaendelea kutekeleza mpango huo na kuwaasa watoto hasa wasichana wajiepushe na vitendo viovu kama vile uasherati ambavyo vinaweza kusababisha kupata mimba na kukatisha ndoto zao za kuendelea na elimu.

Pia alitoa onyo kwa wanaume kuacha tabia ya kuwalaghai watoto hao huku akionya kuwa mtu yoyote atakayekamatwa akifanya mapenzi na mwanafunzi atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Alisema kuwa ni jambo la kusikitisha kuona wilaya ya Namtumbo kwa muda mrefu imekuwa miongoni mwa wilaya zenye rekodi mbaya ya wanafunzi kupata ujauzito na utoro ambapo amewaagiza viongozi wa wilaya hiyo kuhakikisha kwamba wanadhibiti hali hiyo kwa kuwafikisha Mahakamani watuhumiwa ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

No comments: