Wednesday, November 22, 2017

WADAIWA SUGU TTCL KUPANDISHWA KIZIMBANI

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akizungumza na Menejimenti ya kampuni ya simu Tanzania (TTCL) wakati alipotembelea makao makuu ya kampuni hiyo ikiwa ni mara ya kwanza kwake na kuwataka kuwachukulia hatua wale wote wanaodaiwa madeni sugu, upande wa kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Dokta Mary Sassabi.
Na Mwandishi wetu,

NAIBU Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye amesema kuwa wadaiwa sugu ambao hawafuati taratibu za kulipa madeni wanayodaiwa na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) watapelekwa Mahakamani kwa mujibu wa sheria.

Hayo yalisemwa na Waziri huyo alipokuwa katika ziara yake ya kikazi makao makuu ya Ofisi za TTCL jijini Dar es Salaam, akizungumza na Menejimenti ya kampuni hiyo.

Alisema kuwa wale wanaodaiwa ambao hawafuati taratibu za kulipa madeni hayo wanatakiwa wapelekwe Mahakamani kwani wamekuwa wakiendelea kutumia huduma za kampuni hiyo huku wakijua kuwa ni wadaiwa sugu.

Mhandisi Nditiye amesifia huduma ya Conference Video Call inayotolewa na TTCL akieleza kuwa husaidia kupunguza gharama kwa Serikali na kwamba huruhusu watu kufanya mikutano kupitia njia ya mawasiliano na sio kukutana kama ilivyokuwa hapo awali.

“Huduma hii ya Conference Video Call itasaidia kupunguza gharama kwa Serikali ambapo awali ilikuwa unatakiwa kuwakusanya viongozi wote kuja katika mkutano, ila kwa huduma hii unaweza kuzungumza nao wakiwa huko huko waliko”, alisema.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya simu Tanzania, Waziri Kindamba alielezea namna kampuni yao ilivyoweza kukusanya deni la shilingi bilioni 6.8 kwa kipindi cha miezi mitatu kutoka kwa wadaiwa hao huku akifafanua namna mfumo huo wa Conference Video Call unavyoweza kufanya kazi.

Waziri Kindamba aliongeza kuwa hivi sasa TTCL inatekeleza mpango mkakati wa mageuzi ya kibiashara ikiwemo mabadiliko ya kuwa kiongozi wa huduma za mawasiliano na TEHAMA katika soko la Tanzania.

Alisema kuwa wanayo matumaini kuwa mchakato wa kupata sheria mpya ya kampuni hiyo kuja kuwa Shirika la Mawasiliano iliyopitishwa Bungeni wiki iliyopita itakuwa ndiyo kichocheo cha kukua kwa maendeleo ndani ya kampuni.

Hata hivyo kampuni ya TTCL imeweza kukusanya takribani shilingi bilioni 6.8 za madeni ndani ya miezi mitatu kwa wadaiwa sugu ambapo awali deni lilikuwa ni shilingi bilioni 10.7.

No comments: