Sunday, November 19, 2017

HALMASHAURI YASHINDWA KULIPA FIDIA WANANCHI WAREJESHEWA VIWANJA VYAO

Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

HATIMAYE Wananchi wa kata ya Lusonga waliopo katika halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wamerejeshewa viwanja vyao ambavyo vilitwaliwa kwa muda mrefu na halmashauri hiyo kwa makubaliano kwamba watalipwa fidia.

Aidha hatua ya kurejeshewa viwanja hivyo imefuatia baada ya halmashauri hiyo kukosa fedha za kuweza kutekeleza jambo hilo.

Muafaka wa kurejesha viwanja mikononi mwa wananchi wa kata hiyo ulifikia juzi kwenye kikao cha baraza la Madiwani wa mji huo, lilikoketi kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi uliopo mjini hapa.


Hatua hiyo imefikia baada ya Madiwani hao kulalamikia hali hiyo kwa muda mrefu bila kufanyiwa utekelezaji, huku baadhi ya wananchi walianza kuvamia viwanja hivyo na kufanya shughuli zao binafsi kutokana na halmashauri kushindwa kuwalipa fedha zao kwa mujibu wa makubaliano yaliyofanyika hapo awali.

“Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge aliagiza kwamba kama halmashauri haina fedha ya kuwalipa wananchi wale kwa wakati, yale maeneo yarudishwe mikononi mwa wananchi”, alisema diwani wa kata ya Matarawe Leonard Mshunju.

Naye diwani wa kata ya Kitanda Zeno Mbunda aliongeza kuwa ni jambo la busara limefanyika kujadili tatizo hilo mbele ya baraza la Madiwani kwani wananchi wa kata ya Lusonga walifikia katika hatua ambayo sio nzuri kwa lengo la kutaka warejeshewe viwanja vyao.

Hata hivyo hatimaye baraza hilo kupitia Mwenyekiti wake, Kipwele Ndunguru walifikia muafaka kwamba wananchi hao wakabidhiwe viwanja vyao haraka kwa kufuata taratibu husika kutokana na halmashauri hiyo hivi sasa haina fedha za kuweza kuwalipa fidia. 

No comments: