Thursday, May 7, 2015

CUF WAIRUSHIA KOMBORA CCM

Cresencia Kapinga,
Songea.

NAIBU katibu Mkuu bara, Chama Cha Wananchi (CUF) Magdalena Sakaya amewataka wananchi wa Jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma, wafanye mabadiliko kwa kutokipatia kura ya ndiyo Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu ujao, kwa kile alichodai kuwa chama hicho kimekuwa kikiwacharaza bakora za ugumu wa maisha na kuwafanya vijana wazeeke kabla ya wakati wao.

Akihutubia kwenye mkutano wa chama hicho ambao ulifanyika katika viwanja vya Majengo mjini hapa, Magdalena alikirushia kombora CCM akisema kuwa ndio kilichowafikishia wananchi wake ugumu wa maisha waliyonayo sasa watanzania, na kusababisha migogoro na migomo ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara.

Naibu katibu huyo alieleza kuwa hata gharama za maisha hivi sasa zimepanda tofauti na miaka ya nyuma, jambo ambalo mwananchi mwenye kipato cha chini huendelea kuwa masikini na kuteseka na maisha.

“Nikiangalia hapa vijana wengi wa Songea nyuso zenu ni za hazuni tupu, hii inatokana na ugumu wa maisha ambayo yameletwa na chama hiki tawala vijana wengi wamekuwa wazurulaji, wazee hawapati matibabu bure hali kadhalika akina mama wanapokwenda kujifungua hospitali wanapata taabu tu”, alisema Sakaya.


Alifafanua kuwa wakati umefika kwa wakazi wa Songea kufanya mabadiliko na kuachana na sera za Chama cha mapinduzi, kwani mikoa yenye viongozi kutoka vyama pinzani imekuwa na maendeleo makubwa kutokana na CCM imekuwa ikiwahonga wananchi kwa kuwapelekea maendeleo haraka ili waichague.

“Mji wa Songea ni mji mkongwe, lakini miundombinu yenu ni mibovu hata umeme imekuwa ni tatizo upatikanaji wake, maji hakuna na hata huduma za afya imekuwa ni tatizo lazima niwaambie ukweli ndugu zangu, kwa sababu CCM inawafanya nyie kama tenga la kuku ambao mkipewa mahindi mnakula, mchele mnakula wakati umefika sasa wa kufanya mabadiliko ya kweli ili tuweze kuondokana na karaha hizi”, alisema.

Vilevile amewataka wananchi wa Songea watambue kuwa chama hicho tawala, kinawadanganya wananchi wake kama wanavyofanya wauzaji wa pombe haramu aina ya gongo, ambapo wanabadilisha chupa lakini gongo ni ile ile.

Kadhalika amewataka wananchi wa mkoa wa Ruvuma, kujitokeza kwa wingi na kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura ili kila mmoja aweze kwenda kupiga kura muda wa uchaguzi utakapowadia na kwamba endapo hawatatimiza hilo watakuwa wamekosa haki yao ya msingi, ya kupiga kura au kumchagua kiongozi wanayemtaka.


Hata hivyo akiwa katika mkoa huo Naibu katibu Mkuu wa CUF, Sakaya ameweza kufanya mikutano yake katika kata ya Madaba, Songea vijijini na Majengo iliyopo Manispaa ya Songea ambapo ziara yake inaendelea katika wilaya ya Namtumbo na kumalizia wilaya ya Tunduru.

No comments: