Friday, May 29, 2015

WALIOHUSIKA KUCHOMA MOTO BASI KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA


Baadhi ya wananchi wakishuhudia basi la kampuni ya Babu J Trans, likiteketea kwa moto baada ya kuchomwa na wananchi wenye hasira kali.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma imeapa kwamba, haitawasamehe wananchi wa kijiji cha Mhuwesi na Msagula wilayani humo ambao wamehusika kuchoma moto basi la kampuni ya Babu J Trans, na kuliteketeza kabisa kutokana na basi hilo kugonga mtoto na kufariki dunia papo hapo.

Chande Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo, alisema hayo alipokuwa katika eneo la tukio kwa lengo la kujionea uharibifu huo uliofanywa na wananchi wenye hasira kali kwa kujichukulia sheria mkononi, kinyume na taratibu za nchi zinavyotaka.

Mkuu huyo wa wilaya alilaani vikali kitendo hicho, baada ya basi hilo kumgonga mwanafunzi aliyefahamika kwa jina la Faidhi Ally (10) na kusababisha kifo papo hapo, katika ajali iliyotokea Mei 26 mwaka huu majira ya mchana.


Alisema serikali haiwezi kuendelea kuvumilia matukio kama hayo ya uvunjifu wa amani, akidai kuwa ni tukio la tatu sasa kwa wananchi wa maeneo hayo kutekeleza kitendo cha aina hiyo, pale inapotokea ajali kwa kugongwa mtu na kusababisha kifo.

Baadhi ya wananchi wa vijiji hivyo, walikiri kwa nyakati tofauti kushiriki kwa namna moja au nyingine kulichoma moto basi hilo ambalo ni aina ya TATA lenye namba za usajili, T 841 DDL huku wakiiomba serikali iwasamehe juu ya tukio hilo kwamba hawatarudia tena.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela alisema wamejipanga kuhakikisha wanafanya uchunguzi wa kina ili kubaini watuhumiwa wote waliohusika, wanakamatwa na sheria iweze kuchukua mkondo wake.

“Hawa wananchi wenye hasira kali baada ya tukio kutokea, walivamia abiria na kuwaamuru washuke watoke nje ya basi hilo na baadaye kulichoma moto, huku dereva na watu wengine walilazimika kukimbia”, alisema Msikhela.

Kwa mujibu wa abiria waliokuwa wakisafiri na gari hilo, kutoka Songea mkoani Ruvuma kuelekea wilaya ya Masasi Mtwara walisema ajali hiyo ilitokana na uzembe wa marehemu, baada ya kuvuka barabara ghafla wakati basi hilo likipishana na lori ambalo lilikuwa likivuta tela.

No comments: