Sunday, May 24, 2015

WANASIASA SONGEA WADAIWA KUKWAMISHA MPANGO WA TASAF

Na Muhidin Amri,
Songea.

MPANGO wa kunusuru kaya maskini ulioratibiwa na mfuko wa maendeleo ya jamii nchini (TASAF) awamu ya tatu, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma umeweza kuibua kaya maskini 8492 sawa na asilimia 106 ikiwa ni ongezeko la kaya 464 ambazo zilikadiriwa hapo awali kufikiwa na mpango huo, katika Manispaa hiyo.

Aidha hadi sasa TASAF imeweza kutekeleza kazi zake katika mitaa 53 ya mjini hapa, ambayo nayo iliingizwa kwenye mpango kwa lengo la kukabiliana na changamoto zilizopo, hatimaye kuweza kufikia malengo iliyojiwekea.

Mratibu wa mpango wa kunusuru kaya maskini katika Manispaa ya Songea, Christopher Ngonyani alieleza hayo, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake.


Ngonyani alidai kuwa uhaulishaji wa miradi ya mfuko huo, katika baadhi ya maeneo unakwamishwa na wanasiasa ambao huwadanganya wananchi wasishiriki katika utekelezaji wake, jambo ambalo aliongeza kuwa linahatarisha kurudisha nyuma jitihada zinazofanywa na serikali katika kupunguza umaskini na ajira kwa wananchi.

Mbali na hayo, kumekuwa pia na tatizo kwa baadhi ya kaya ambazo ziliandikishwa kwenye mpango huo wa TASAF kwa ajili ya kufanyiwa utekelezaji, baadhi yao wamekuwa wakihama makazi yao kutoka sehemu moja kwenda nyingine kitendo ambacho husababisha kukosekana kwa mlengwa, ambaye aliandikishwa katika eneo lake na kufanya akose huduma husika.

Pia Mratibu huyo anaiomba jamii kuachana na maneno ya wanasiasa ambao wanaonesha kutokuwa na nia njema kwao, badala yake washiriki kikamilifu ili kuweza kunusuru kaya ambazo huishi katika mazingira hatarishi ili kutimiza adhima ya serikali, kuwafikia walengwa wote waliopo kwenye mpango huo.


Kadhalika amewataka kujenga tabia ya kuhudhuria mara kwa mara katika shughuli zote ambazo zimepangwa na TASAF, ikiwemo kufanya ufuatiliaji wa tarehe za malipo ya fedha zao na kujihusisha kwenye kazi sambamba na kuchangia nguvu zao ili miradi iliyopangwa, iweze kufikia malengo na kukamilika kwa wakati uliopangwa.

No comments: