Saturday, May 23, 2015

GOLD STAR YAWAJENGEA UWEZO MAFUNDI RANGI RUVUMA

Na Julius Konala,
Songea.

MAFUNDI rangi waliopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wamenufaika na mafunzo juu ya utumiaji wa tekinolojia ya upakaji rangi ikiwa ni lengo la kuwajengea uwezo, utendaji wa kazi zao za kila siku.

Zaidi ya mafundi 100 ndio waliopewa mafunzo hayo na kampuni ya Gold Star katika Manispaa hiyo, ambayo yalifanyika kwa muda wa siku moja kwenye ukumbi wa chuo cha Top one inn, mjini Songea ambayo yalishirikisha wanawake na wanaume.

Akizungumza katika mafunzo hayo Meneja mauzo wa kampuni hiyo, Ally Khalfan alisema kuwa lengo ni kuboresha taaluma ya upakaji rangi kwa mafundi hao, ili kuweza kuleta mabadiliko katika utendaji wa kazi zao.


Meneja huyo alieleza kuwa mafundi wengi hapa nchini, wamekuwa wakifanya kazi ya upakaji rangi kienyeji na kwa kiwango cha chini bila kuzingatia vigezo husika, jambo ambalo kampuni yake lilimfanya aweze kujenga msukumo wa kuendesha mafunzo hayo ili mafundi hao waweze kujiajiri wao wenyewe katika shughuli mbalimbali za upakaji rangi, pale zinapojitokeza na kwa viwango vinavyokubalika.

Naye Mkurugenzi wa chuo cha Top one inn kilichopo mjini hapa, Paschal Msigwa aliwataka washiriki wa mafunzo hayo huko waendako mara baada ya kupatiwa ujuzi huo wa namna ya upakaji rangi, wakafanye mabadiliko sahihi katika kazi zao ambayo yataleta faida kwao na taifa kwa ujumla.

Awali alipokuwa akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Meya wa Manispaa ya Songea, Diwani wa kata ya Mshangano mjini hapa, Faustine Mhagama aliishukuru kampuni ya Gold Star kwa uamuzi wake wa kuwajengea uwezo mafundi rangi kwa kile alichoeleza kuwa, ni nafasi pekee itakayowafanya wengi wao waweze kujiajiri wenyewe.


Mhagama alisema kuwa elimu waliyoipata huko waendako, wakiitumia vizuri itaweza kusaidia na kuboresha upakaji rangi katika nyumba na majengo mbalimbali kwa viwango vinavyokubalika, badala ya kufanya kazi kienyeji kama ilivyokuwa hapo awali.

No comments: