Friday, May 29, 2015

NALICHO: WANANCHI TUSHIRIKIANE KUWAUA SIMBA

Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Chande Nalicho akizungumza na wananchi wa wilaya hiyo katika moja ya ziara yake ya kikazi ambazo amezifanya hivi karibuni.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHANDE Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, amewataka wananchi wa vijiji vilivyopo katika tarafa ya Matemanga wilayani humo kutumia nguvu zao na kujituma kwa hali na mali, kuhakikisha kwamba simba ambao wamekuwa wakiwasumbua hasa nyakati za usiku wanauawa ili wananchi waondokane na adha wanayoipata sasa ya kushindwa kuishi kwa amani.

Nalicho alitoa kauli hiyo, alipokuwa akikabidhi askari wa nane idara ya wanyamapori wilayani humo, ambao walipelekwa katika tarafa hiyo kwa lengo la kupambana na simba hao kuhakikisha kwamba wanauawa.

Hatua hiyo imefuatia kutokana na simba hao wamekuwa wakishambulia mifugo ya wananchi hasa nyakati za usiku, jambo ambalo linahatarisha hata usalama wa binadamu kwa wakazi wanaoishi katika vijiji vilivyopo kwenye tarafa ya Matemanga.


Awali akitoa taarifa ya matukio hayo Mtendaji wa kata ya Matemanga, Omary Hussein alieleza kuwa simba hao ambao walianza kuleta madhara katika makazi ya watu mapema mwezi Februari mwaka huu, wamekwisha poteza uhai wa mbuzi 25, mbwa 3 pamoja na kujeruhi ng’ombe 2.

Omary alifafanua kuwa pamoja na serikali kupeleka mara kwa mara askari wanyama pori, lakini bado jitihada za kuwaua wanyama hao wakali hazijazaa matunda na bado wananchi wa maeneo hayo, wanaendelea kuishi kwa hofu kubwa.

Nao wananchi ambao walizungumza kwa nyakati tofauti walisema kuwa mbali ya maelekezo ya viongozi kutolewa, yakiwataka wananchi kulala mapema na kupunguza safari nyakati za usiku wamekuwa sasa wakilazimika kulala na makopo makubwa ndani ya nyumba zao, ambayo huyatumia kujisaidia usiku kutokana na kuogopa kwenda nje ya nyumba zao ambako wamejenga vyoo, wakihofia kutafunwa na simba.

Akizungumza katika mkutano huo, Afisa ardhi na maliasili wa wilaya ya Tunduru Japhet Mnyagala aliwahakikishia wananchi kuwa idara yake itaendelea na msako mkali wa kuwaua wanyama hao wakali, mpaka pale tatizo hilo litakapokuwa limekwisha.


Mnyagala alisema awamu hii askari wake, wamejiandaa na wanarisasi za kutosha hivyo mafanikio ya kuwaua watashirikishwa wazee wa mila ambao watawasaidia wakati wa kutekeleza zoezi hilo, kutengeneza na kutega hata mitego ya asili ambayo inaweza kufanikisha kuwakamata kwa urahisi zaidi.

No comments: