Friday, May 22, 2015

MADIWANI WATAKIWA KUTOWAOGOPA WATUMISHI

Na Kassian Nyandindi,
Namtumbo.

MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wametakiwa kutowaogopa watumishi na watendaji wa serikali waliopo katika wilaya hiyo, badala yake wawabane na kuwahoji ikiwemo hata kufanya ufuatiliaji wa fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi, ambazo hupelekwa katika maeneo yao.

Mbali na hatua hiyo, pia wamehimizwa kuwashirikisha wananchi ili  nao waweze kushiriki vyema katika shughuli za miradi hiyo jambo ambalo litawezesha wilaya, kufikia malengo yake iliyojiwekea ikiwemo kupiga hatua katika nyanja ya kiuchumi.

Rai hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Stephen Nana alipokuwa akizungumza na watumishi pamoja na madiwani katika kikao cha baraza la madiwani, ambacho kiliketi mjini hapa.


Nana alisema ni lazima madiwani waache tabia ya kuwanyenyekea watumishi wa serikali, hata kama wanakabiliwa na hali ngumu ya kimaisha ambapo aliongeza kuwa woga wao utatoa nafasi kwa watumishi hao, kufanya kazi kwa mazoea na kusababisha hasara kwa taifa hili.

Kadhalika alieleza kuwa ufuatiliaji juu ya matumizi sahihi ya fedha za miradi ni jambo la lazima lisilo na mjadala, kwani kufanya hivyo kutasaidia fedha hizo  kutekeleza majukumu yaliyokusudiwa ikiwemo kuimarisha hata baadhi ya miundombinu na huduma za kijamii.

Alifafanua kuwa baadhi ya madiwani wa halmashauri ya Namtumbo wamekuwa kikwazo kikubwa kwa kutotimiza majukumu yao ya kazi ipasavyo, kitendo ambacho kinahatarisha kudorola kwa maendeleo ya wilaya hiyo na kusababisha jamii kuendelea kuwa masikini.

“Hakuna pingamizi lolote kwa diwani kuhoji au kufuatilia matumizi ya fedha za maendeleo zinazoletwa na serikali kwa ajili ya mradi fulani katika kata au wilaya, isipokuwa ni lazima ufuatiliaji ufanyike kikamilifu kwenda katika eneo la mradi ili kuweza kubaini ubora wa mradi husika, mkifanya hivyo mtafanya utekelezaji wake uwe katika viwango”, alisema Nana.


No comments: