Sunday, November 22, 2015

MAGUFULI AOMBWA KUINGILI KATI MIGOGORO YA WAFUGAJI TUNDURU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Magufuli.


Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAFUGAJI jamii ya Kisukuma, wanaoendesha shughuli zao za ufugaji wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma wamemuomba  Rais wa awamu ya tano, Dokta John  Magufuli, kuwasaidia kudhibiti migogoro ya wafugaji na wakulima ambayo inaendelea wilayani humo.

Hayo yalisemwa na wafugaji hao, katika sherehe ya kumpongeza Dokta Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, zilizofanyika kwenye kambi yao ya wafugaji iliyopo kijiji cha Masonya wilayani hapa.

Kiongozi wa wafugaji hao Lugwasha Mtegwambuli, alisema kuwa kufumbiwa macho kwa migogoro hiyo ambayo imedumu kwa muda mrefu sasa, imekuwa ikigharimu maisha yao na kuwafanya waishi kama wakimbizi.

“Tunampongeza Dokta Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Tanzania, tunaimani naye kubwa katika utendaji wake wa kazi ili wananchi aweze kutufikisha katika maendeleo ya kweli”, alisema Mtegwambuli.


Aidha alimuomba Rais Magufuli, kuimarisha usalama kati ya wananchi na wawekezaji tofauti na sasa ambapo baadhi yao wamekuwa wakikiuka taratibu na kuleta madhara kwa jamii, zinazowazunguka katika maeneo yao ya wafugaji.

Mtegwambuli alisema kuwa wapo baadhi ya wawekezaji wamekuwa wakijifanya miungu watu, wamekuwa wakitoa adhabu kali kwa wananchi wanaowazunguka pindi inapotokea wameingia katika maeneo ya miradi yao.

Alifafanua kuwa wamekuwa wakipata madhara makubwa, ikiwemo watu na mifugo yao huku wengine wakipoteza maisha kwa kupigwa risasi kwa madai kwamba, wanaingia katika maeneo ya miradi ya hifadhi bila kibali maalum.

Kiongozi huyo wa wafugaji wilayani Tunduru alieleza kuwa, endapo serikali haitaweka mikakati ya kudumu juu ya kumaliza tatizo hilo, uwezekano wa kuondoka  kwa manyanyaso dhidi ya jamii hizo hayatakoma badala yake yatakuwa yakiendelea na kuathiri jamii. 
 
Naye Thomas Matindi, ambaye ni mfugaji kijiji cha Kidodoma wilayani humo pamoja na mambo mengine  aliiomba serikali  kuwatambua wafugaji kwani wamekuwa kwa kiasi kikubwa wakichangia pato la Taifa, kupitia mifugo yao.

Mwenyekiti wa kijiji hicho, Khalifa Makunganya alisema kuwa katika kipindi chote wamekuwa wakiishi vizuri na wafugaji hao na kwamba, wamekuwa wachangiaji wazuri katika shughuli mbalimbali za maendeleo.

Wafugaji hao ambao kwa sasa takribani wana ng'ombe 28,000 wilayani Tunduru, walianza kufanya shughuli hizo wilayani humo mwaka 2007 baada ya serikali kuwaondoa katika bonde la Ihefu mkoani Mbeya, kwa lengo la kuwapeleka katika mikoa ya Lindi na Mtwara ambapo walibakia hapa wilayani, baada ya tamko la serikali la kuwataka wabakie katika maeneo hayo ili kuepusha homa ya Bonde la ufa iliyozuka wakati wakiwa safarini kuelekea katika mikoa hiyo.

No comments: