Thursday, November 12, 2015

VIONGOZI TUNDURU WATAKIWA KUJENGA USHIRIKIANO NA WANANCHI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

VIONGOZI waliopo katika vijiji na kata wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameaswa kujenga ushirikiano kwenye vikao vyao vya maamuzi mbalimbali ya kimaendeleo, ili waweze kuisaidia wilaya hiyo kufikia malengo na utekelezaji wa ahadi zilizoahidiwa na viongozi wao, wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ambao umefanyika Oktoba 25 mwaka huu.

Hayo yalisemwa na Madiwani wateule kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao wamepewa ridhaa ya kuingia katika baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya hiyo, wakati walipokuwa wakitoa shukrani zao kwa kuchaguliwa katika sherehe zilizofanyika kata ya Matemanga wilayani humo. 

Diwani mteule kutoka kata ya Marumba, Msenga Said Msenga alisema kuwa endapo wananchi hawatashiriki ipasavyo katika shughuli za maendeleo, mafanikio yatachelewa kuwafikia katika maeneo yao hivyo wanapaswa kujenga ushirikiano wa kutosha, ili kuweza kufikia malengo husika. 


Alisema kuwa diwani kazi yake sio kubuni na kupeleka miradi katika vikao peke yake, bali kazi yake ni kukaa na wananchi wake kupitia vikao vya (WADC) na kujenga hoja za uibuaji wa miradi hiyo na kufanya ufuatiliaji ikiwemo pia kusimamia miradi, ambayo imeibuliwa na kuipeleka ngazi ya juu kwa ajili ya utekelezaji. 

“Nawaomba viongozi tuwashirikishe wananchi kwa kufanya nao vikao vya kupitisha maamuzi mbalimbali, sio kukaa mezani na kutengeneza mambo ambayo wananchi hawajashirikishwa”, alisema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Tunduru, Hamis Kaesa akatumia nafasi hiyo kuwaomba viongozi kuwashirikisha wananchi wakati wa uibuaji wa miradi husika, na kuisimamia wakati wa kuipitisha katika vikao vya maamuzi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Katibu mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Tunduru,  Aindi Daruweshi pamoja na kuwapongeza wananchi kwa  maamuzi hayo, alikiri kuwa chama chake kilipata wakati mgumu walipokuwa kwenye kampeni za uchaguzi huo.

Daruweshi alisema kuwa ugumu huo, ulitokana na uwepo wa wanachama mamluki ambao walikuwa sio waaminifu ndani ya chama.

Alitamba akisema kuwa katika uchaguzi huo, chama hicho kimeibuka kidedea katika majimbo ya ubunge yaTunduru kusini na kaskazini, ambapo kilipata madiwani 26 kati ya kata 39 zilizopo katika majimbo hayo.

No comments: