Saturday, November 14, 2015

UTARATIBU WA KISHERIA UNAPOTAKA KUNUNUA ARDHI YA KIJIJI



Na Bashir Yakub,

TULIPOANDIKA namna  bora  na  taratibu  maalum  za  kufuata unapotaka  kununua  ardhi,  tulisema  pia taratibu  za  ununuzi  wa  ardhi  huwa  zinatofautiana kutegemea  na   mazingira  ya  kila  ardhi. Tukasema  unaponunua  ardhi  kwa  msimamizi  wa  mirathi,  ni  tofauti  na  unaponunua  kwa  mmiliki  mwenyewe.

Unaponunua  ardhi  ya  familia  ni  tofauti  na  unaponunua  isiyo  ya  familia. Vilevile  unaponunua  ardhi  ya  kijiji  ni  tofauti  na  unaponunua ardhi  isiyo  ya  kijiji. Taratibu  hutofautiana  na  hasa  tofauti  ipo  katika  nyaraka  ambazo  zinatakiwa  kuambatanishwa,  ikiwa  kama  ithibati  ya  ununuzi. Hata  uandishi  wa   mkataba  wa  manunuzi  pia  nao huwa na tofauti  katika  hili.

1. ARDHI  YA  KIJIJI  KWA  UWEKEZAJI.

Wako  watu  wamekuwa   wakinunua  ardhi  hasa  huko  vijijini,  lakini  baadae  wamekuwa  wakijikuta  katika  migogoro  mikubwa  na  wenyeji. Mwamko  wa  kununua  maeneo  kama  Bagamoyo, Kisarawe, huko  Chanika  Dondwe na  maeneo  mengine  umekuwa  mkubwa  sana. Hata  hivyo  mwamko  unavyoongezeka  ndivyo  na  migogoro  inavyoongezeka. Kubwa katika  migogoro  hii  ni  hatua  ya  wanunuzi  kutokufuata  utaratibu  wa  ununuzi aidha  kwa  kujua, kutokujua  au  kupotoshwa.

Wakati  mwingine  ni  uelewa mdogo  miongoni  mwa  wenyeji,  lakini  zaidi  ni  hili  la  kutofuata utaratibu. Mara  zote  huwa  tunasema  ni  bora  zaidi  mgogoro  unapotokea  halafu  ukukute  ulifuata  taratibu  wakati  wa  manunuzi. Bila  shaka hautakuwa  na  athari  kubwa  kwako,  lakini  ni  mbaya   zaidi  ukitokea  halafu  ukukute kuna  taratibu  hukufuata kwa  bahati  mbaya  au  bila  kujua. Unakuwa  katika  hatari  ya  kupoteza. Unapokwenda  kununua  ardhi  ya  kijiji  kwasababu  yoyote  ile  hasa uwekezaji,  upo  utaratibu maalum wa kufuata  nitakaoeleza.

2. ARDHI  YA  KIJIJI  NI  NINI.

Ardhi  ya  kijiji  ni  ile  ardhi  iliyopo  katika  mipaka  ya  kijiji  fulani,  ilyoainishwa  na  mamlaka  za  wilaya  husika  huku  ikiwa  na  hati ya  usajili  wa  kijiji. Ardhi  hii  hulindwa  kwa  taratibu  za  kimila  za  eneo  husika,  ikiwa  ni  pamoja  na sheria  namba  4 ya  1999.

3. UTARATIBU  WA  KUNUNUA  ARDHI  YA  KIJIJI  KISHERIA.

( 1 ) Maombi  maalum huandaliwa  na  kuwasilishwa  kwa  mtendaji  wa  kijiji  ambaye  hupatikana  katika  kila  kijiji.

( 2 ) Maombi  huandaliwa  katika  fomu  maalum  ambazo  hupatikana  katika  kila  ofisi  za  kijiji. Si  maombi  ambayo  huandaliwa  kama  barua  za  kawaida za maombi.

( 3 ) Ikiwa  mwombaji  ni  mtu  mmoja   basi   atasaini  sehemu  maalum  na ikiwa  ni  maombi  kwa  niaba  ya  famliia,  basi  watu  wawili  kutoka  ile  familia  watasaini  na  ikiwa  ni  ardhi  kwa  ajili  ya  kikundi  pia  wawakilishi  wasiopungua wawili  kutoka  kila  kikundi  watasaini  kwa  niaba  ya  wengine.

( 4 ) Kama  mwombaji  ni  chama  cha  ushirika  au  kampuni,  basi  inatakiwa  kuwepo  wadhamini  wawili   kwa  ajili  ya  shirika  au  kampuni  hiyo. Wanaweza  kuwa  zaidi  ya  wawili  lakini  wasipungue.

( 5 ) Kama  anayeomba  ardhi  si  mwenyeji  wa  eneo  husika,  basi  atatakiwa  kuwa  na  wadhamini  wasiopungua  watano  ambao  ni  wenyeji  wa  eneo  hilo. Sharti  ni  kwamba  kati ya  hao  wadhamini  wasiwepo  ndugu  wa  mwombaji.

( 6 ) Mwombaji  atatakiwa  kuambatanisha katika  maombi  yake  tamko  linaloonesha  ardhi  nyingine  anayoimiliki  Tanzania  nje  na  hiyo  anayoomba.

( 7 )  Ikiwa  ardhi  inaombwa  kwa  ajili  ya  makazi  basi  mwombaji  atatakiwa  kuambatanisha  tamko  linaloonesha  kuwa  ataanza  ujenzi wa  makazi hayo ndani  ya  miezi  mitatu  tangu  siku  ya  kuidhinishiwa  ardhi.

( 8 ) Ikiwa  mauzo  ni ekari 50 au  kuendelea  ni lazima  yaidhinishwe  na  mkutano  mkuu  wa  kijiji.

( 9 ) Baada  ya  kukamilisha  taratibu  hizo  halmashauri  ya  kijiji  itakaa  vikao  na  ndani  ya  siku  tisini itatakiwa  kutoa  majibu.

Kamwe  usikubali  kuuziwa  ardhi  ya  kijiji  na  viongozi   wa  kijiji,  bila  kufuata  utaratibu  huu. Hii  hasa  ni kwa  wawekezaji  wanaochukua  maeneo  makubwa  kwa  shughuli  za  kiuchumi. 

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,     0714047241              bashiryakub@ymail.com

No comments: