Wednesday, March 2, 2016

APANDISHWA KIZIMBANI KWA KUKUTWA NA SILAHA



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MKAZI mmoja wa kijiji cha Chiwana wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, Sanane Chigadula (75) amepandishwa kizimbani, katika Mahakama ya wilaya hiyo kwa tuhuma ya kukutwa na bunduki tatu na risasi.

Akisomewa shitaka mbele ya Hakimu wa Mahakama ya wilaya ya Tunduru, Gladys Barthy, Mwendesha mashitaka mkaguzi msaidizi wa Polisi inspekta Songelael Jwagu alisema kuwa mtuhumiwa huyo, alikutwa na  silaha hizo katika kijiji cha  Chiwana Februari 4 mwaka huu majira ya jioni.

Katika tukio hilo alisema kuwa, Chigadula alikutwa akiwa na bunduki aina ya  Rifle 2, ikiwa ni ya kisasa moja na  iliyotengenezwa kienyeji moja.

Inspekta Jwagu alifafanua kwamba, pia katika tukio hilo mtuhumiwa huyo alikutwa akiwa na bastola moja aina ya Revova  yenye risasi zake tatu.


Mahakamani hapo ilielezwa kuwa,  kitendo hicho cha kumiliki bunduki hizo bila ya kuwa na kibali alifanya kosa kinyume cha sheria za nchi namba 4 (1) cha kanuni ya adhabu sura ya 223 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Mtuhumiwa alikana mashitaka yote, alipelekwa rumande kutokana na upelelezi kutokamilika hivyo shauri lake, litatajwa tena Marchi 8  mwaka huu.

No comments: