Wednesday, March 9, 2016

MADIWANI TUNDURU WASUSIA KIKAO CHA BAJETI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MADIWANI wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) wilaya ya Tunduru mkoa wa Ruvuma, wamesusia kuendelea na kikao cha kupitisha rasimu ya bajeti ya halmashauri ya wilaya hiyo, wakidai kuwa kumekuwa na tatizo la uchakachuaji mkubwa wa miradi ya wananchi wilayani humo.

Aidha walisema kuwa wameamua kufanya hivyo kutokana na kikao hicho kucheleweshwa kufanyika, huku sababu za msingi za kuchelewa huko hazijulikani.

Hayo yalisemwa na madiwani hao, katika mahojiano maalumu yaliyofanyika baada ya kutoka nje ya kikao hicho huku wakiongeza kuwa viongozi wa halmshauri hiyo baadhi yao wamekuwa hawatekelezi majukumu yao ya kazi ipasavyo, ikiwemo suala la ujenzi wa miradi ya wananchi.

Madiwani hao ambao wapo 16 kutoka katika vyama vinavyounda UKAWA wilayani Tunduru, walisema kilichowakera hasa ni kitendo cha kuchelewa kuanza kwa kikao hicho wakiwa wanamshinikiza Mwenyekiti wao, Mkwanda Sudi ili awaeleze ni sababu gani iliyowafanya wachelewe kuanza kwake sababu ambazo hazikutolewa.


Naye diwani wa kata ya Kidodoma, Rashid Choga alisema kuwa kitendo hicho kilifanywa na madiwani wa Chama Cha Mapinduzi, kwa lengo la kupanga njama za kuwahujumu madiwani wa vyama pinzani, kwani bajeti hiyo ilikuwa haioneshi uwepo wa miradi mipya katika maeneo ya kata zao.

Diwani wa kata ya Mlingoti mashariki, Aloyce Nyoni alisema kuwa katika kikao hicho walipanga pia kufichua wizi na ufisadi unaofanywa na viongozi wa Tunduru, kupitia makusanyo ya ushuru wa stendi kuu ya magari ya abiria iliyopo wilayani humo.

Vilevile alisema kuwa walipanga kuhoji mapato yatokanayo na ushuru wa soko kuu la Azimio lenye wafanyabiashara zaidi ya 200, lakini mapato yake hayawekwi wazi ili wananchi waweze kutambua halmashauri yao inakusanya kiasi gani.

Naye Diwani wa kata ya Ngapa, Said Pindu alisema kuwa katika bajeti hiyo alipanga kuhoji kutowekwa kwa mradi wa ujenzi wa shule ya msingi Ngapa ambayo ilipata maafa na kubomoka Januari 5 mwaka 2014, jambo ambalo linasababisha wanafunzi wa shule hiyo kusomea chini ya miti.

Alisema katika kata yake kuna uhaba mkubwa wa maji safi na salama, kitendo ambacho kinawafanya wananchi wake kunywa maji machafu kutoka katika mito.

Diwani wa kata ya Nakapanya Kubodola Ambali, alisema kuwa katika kikao hicho alijipanga kuhoji juu ya kata yake, kudorola kwa mradi wa uchimbaji wa kisima uliogharimu shilingi milioni 300 zilizotolewa na serikali kupitia ufadhili wa benki ya dunia.

Alisema katika mradi huo jumla ya shilingi milioni 12 zilitolewa kwa ajili ya kufanya kazi hiyo, na kwamba kinachomshangaza mradi huo umetelekezwa lakini maji hayatoki.
Alisema pia katika kata yake kulikuwa na mradi wa ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 9 kutoka katika kijiji cha Nakapanya kwenda kijji cha Tuliyeni, ukiwa umepangwa kugharimu shilingi milioni 15 lakini haujakamilika hadi sasa na awamu hii haujawekwa katika mpango wa bajeti yao.

Akitoa taairfa ya makadirio ya rasimu hiyo ya bajeti ambayo ilikuwa ikipitishwa na madiwani wa upande wa chama kimoja cha siasa, Kaimu Ofisa mipango wa halmashauri ya Tunduru Rudrick Charles alisema kuwa shilingi bilioni 55,563,326,655.00 zitatokana na vyanzo vya mapato ya ndani na ruzuku kutoka serikali kuu.

Charles alisema kwamba kati ya fedha hizo, kiasi cha shilingi 2,589,643.00 zitatokana na mapato ya ndani na shilingi 52,973,684,655.00 zitatokana na ruzuku kutoka serikali kuu na wadau wa maendeleo.

No comments: