Wednesday, March 9, 2016

MKAGUZI WA NDANI OFISI YA MKUU WA MKOA RUVUMA ASHIKILIWA NA TAKUKURU

Yustina Chagaka, Mkuu wa TAKUKURU mkoani Ruvuma.


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

PHILIMON Lenard ambaye ni Mkaguzi wa mahesabu ya ndani, Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, anashikiliwa na kuhojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani humo, akidaiwa kuhusika na vitendo vya rushwa katika utendaji wa kazi zake za utumishi wa umma.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda wa TAKUKURU  mkoani Ruvuma, Yustina Chagaka alisema kuwa Lenard alikamatwa Machi 4 mwaka huu majira ya mchana, baada ya ofisi yake kupata taarifa kutoka  kwenye vyanzo mbalimbali kuhusiana na vitendo vya rushwa alivyokuwa akivifanya.


Chagaka alisema kuwa tokea siku aliyokamatwa mpaka sasa, bado wanamshikilia wakiendelea kumhoji  na kupekuliwa ili kuweza kubaini ukweli wa taarifa ambazo wamezipokea kuhusiana na mwenendo wake wa kazi na vitendo vya rushwa na kwamba wakimaliza zoezi hilo, atachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

“Hivi sasa tunaendelea kumhoji na kumfanyia uchunguzi wa kina hivyo hatuwezi kuwapa taarifa yoyote au malalamiko tuliyoyapokea kutoka kwenye vyanzo vyetu mpaka tukamilishe zoezi hili, subirini kazi hii tunayoifanya ikamilike ni mapema mno kutoa taarifa hizi mambo yote yatakuwa bayana, hivi sasa uchunguzi bado unaendelea”, alisema Chagaka.

Hata hivyo Kamanda huyo wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa hapa mkoani Ruvuma, alitoa mwito kwa wananchi kujitokeza kutoa taarifa yoyote inayohusiana na vitendo vya rushwa, ambavyo hufanywa na mtu yeyote kwani endapo watafanya hivyo wataiwezesha taasisi hiyo kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi na kukomesha hali hiyo isiweze kuendelea kuathiri jamii.

No comments: