Wednesday, March 2, 2016

UZALISHAJI ZAO LA MPUNGA WILAYA YA NAMTUMBO WAONGEZEKA



Na Kassian Nyandindi,
Namtumbo. 

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Chande Nalicho amesema kwamba uzalishaji wa zao la mpunga katika wilaya hiyo umeongezeka  kutoka tani 50,000 mwaka 2012 sawa na  tani 2 kwa hekta, hadi kufikia tani 143,375 kwa mwaka  2015 ambayo ni wastani wa tani 4  kwa  hekta moja, jambo ambalo limeifanya wilaya hiyo kukua kiuchumi na kupunguza  umaskini kwa wananchi wake.
Zao la Mpunga.

Ongezeko hilo la uzalishaji  alifafanua kuwa limetokana na zao hilo kuwa la kibiashara zaidi,  hasa baada ya kupatikana kwa soko kubwa mikoa jirani ya Lindi na Mtwara ambako mahitaji ya  mchele ni makubwa  ikilinganishwa na matumizi yaliyopo  ndani ya wilaya hiyo, hivyo kuwepo kwa wafanyabiashara wengi wanaokwenda kununua na kufanya thamani ya zao hilo kukua.


Nalicho  alisema hayo alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofisini kwake, kuhusiana na hali  ya  chakula  na shughuli za maendeleo, katika sekta ya kilimo zinavyoendelea wilayani humo.

Aidha alieleza kuwa, kuongezeka kwa  skimu ya kilimo cha umwagiliaji na matumizi ya mbolea na zana bora za kilimo  chini ya mpango madhubuti wa kuongeza uzalishaji wa chakula na mazao ya  biashara, unaofanywa na halmashauri ya wilaya hiyo ndiyo umeleta ufanisi mkubwa katika uzalishaji wa zao la mpunga na kuifanya wilaya ya  Namtumbo, kujitosheleza kwa chakula ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

Katika msimu wa kilimo wa mwaka 2014/2015 hekta 251,431.3 kati ya hekta 263.369 ndizo zilizopangwa kulimwa, ambazo zingeweza kuzalisha tani 450,631.4 kati ya malengo  ya kuzalisha tani 500,174.4 ambazo  walishindwa kuzifikia kutokana na uwepo wa changamoto mbalimbali.

Changamoto  hizo alizitaja kuwa ni huduma duni za usambazaji wa pembejeo, miundombinu hafifu ya umwagiliaji  na pembejeo hizo kuuzwa kwa bei ghali, ambayo wakulima wengi walishindwa kumudu gharama husika.

No comments: