Monday, March 21, 2016

CCM RUVUMA KUANZA KUTUMBUA MAJIPU YAWATAKA WATENDAJI WAKE KUFANYA KAZI KWA UADILIFU

Upande wa kushoto, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Ruvuma Oddo Mwisho akimpatia mmoja wa wanachama wa UWT cheti cha pongezi na shukrani, baada ya kuongoza na kufanya kazi vizuri ndani ya jumuiya hiyo.


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Ruvuma, Oddo Mwisho amesema kwamba katika baadhi ya maeneo mkoani humo watendaji wake ndani ya chama, wamekuwa sio waaminifu kwenye matumizi ya fedha hivyo kufuatia kuwepo kwa hali hiyo wamejipanga kuwachukulia hatua ili kuweza kunusuru hali hiyo isiweze kuendelea na kuwaondoa hofu wanachama wa chama hicho.

Aidha alisema kuwa fedha hizo ni zile ambazo zinatolewa na jumuiya za chama na michango kutoka wadau mbalimbali, kwa ajili ya kukiendeleza chama. 

“Nawataka watendaji wafanye kazi kwa uadilifu mkubwa, ondoeni usumbufu ndani ya chama tumikieni chama kwa moyo wote na sio kuwa watu wa kubadilika, watu kama hawa hatuwahitaji ndani ya chama”, alisema Mwisho.

Mwenyekiti huyo alisema hayo jana kwenye kikao cha wajumbe wa baraza la wanawake wa CCM mkoani Ruvuma, ambacho kilifanyika kwenye ukumbi wa chama hicho mkoani humo.

Alisema kuwa uongozi wa mkoa huo ndani ya chama umekaa na kubaini kwamba, katika maeneo yake kuna watendaji ambao sio waaminifu na ni majipu ambayo inabidi yatumbuliwe ili kuweza kuleta heshima, kwa kuwapa adhabu ya kuwafukuza kazi na nafasi zao kuzibwa na wengine wenye kuzingatia maadili ya kazi ndani ya chama.


“Tumekwisha anza kukaa kwenye vikao kwa ajili ya kuwashughulikia hawa watu, nachukua nafasi hii kuwaasa pia katika wilaya zetu mnapoona kuna matatizo kama haya, wafikisheni kwenye vikao watumbueni msiwaonee haya”, alisema.

Alisema kuwa ni lazima washirikiane na viongozi wa jumuiya zao, ili kuhakikisha ufanisi mzuri wa utekelezaji wa matumizi mazuri ya fedha na kuweza kuondoa dhana potofu iliyojengeka kwa baadhi ya wadau, ambao ni wachangiaji wa fedha kwa lengo la kukikuza chama kiuchumi.

Vilevile alisisitiza kwa kuwataka huko waendako wakahamasishe wenzao kuiimarisha vikundi vyao vya ujasiriamali kiuchumi ili mkoa wa Ruvuma, uweze kusonga mbele kimaendeleo kwa manufaa ya jamii.

Awali akisoma taarifa fupi ya maendeleo ya Umoja Wanawake Tanzania (UWT) mkoani humo Katibu wa  jumuiya hiyo, Chiku Masanja alisema kuwa wanampongeza Rais John Magufuli kwa kuthubutu kufanya kazi kwa kujituma kwa moyo na kuifanya nchi iweze kusonga mbele, katika sekta mbalimbali za kukuza uchumi na kuijengea heshima serikali ya awamu ya tano.

Pia Masanja aliwataka wanawake wenzake kwenye jumuiya hiyo, kuvunja makundi yasiyokuwa ya lazima ili waweze kufikia malengo yaliyokusudiwa na kufanya shughuli za uzalishaji mali, ambazo zitawafanya waweze kuondokana na dhana ya kuwa tegemezi au omba omba.

No comments: