Thursday, March 3, 2016

WATAKIWA KUSIMAMIA KIKAMILIFU UKUSANYAJI WA MAPATO



Na Mwandishi wetu,
Namtumbo.

VIONGOZI kuanzia ngazi ya vijiji na kata  wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wamekumbushwa wajibu wao katika kusimamia kikamilifu ukusanyaji ushuru na mapato mengine ya  serikali, na sio kazi hiyo kuiacha ifanywe na wazabuni ambao wengi wao wanatoa taarifa za uongo na kuikosesha halmashauri ya wilaya hiyo mapato yake.

Imeelezwa kuwa endapo watafanya hivyo, hatua hiyo itasaidia  kuongeza mapato ya halmashauri na kuwa na uwezo wa utekelezaji  wa miradi na shughuli nyingine za maendeleo, kwa manufaa ya wananchi.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo,  Danny Nyambo  alisema hayo mjini hapa alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ambapo  amemtaka kila mtumishi ndani ya halmashauri hiyo, kujipima mwenyewe kiutendaji na kama anaweza kumudu kasi ya utendaji kazi wa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na kauli mbiu ya Hapa kazi tu.


Nyambo amempongeza Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo, Ali Mpenye kutokana na   ufuatiliaji wake na usimamizi mzuri wa fedha za ushuru wa mazao  na kuweza halmashauri hiyo kwa mara ya kwanza kukusanya, shilingi milioni 150 kwa mwezi.

Alisema kazi ya ukusanyaji  na usimamizi wa fedha, isiachwe kwa mtu mmoja bali kila mtumishi anatakiwa kuwa mpambanaji namba moja katika kusimamia suala hilo kikamilifu.

Kufuatia kuwepo kwa ukusanyaji na udhibiti mzuri wa vyanzo vya mapato wilayani humo, kunaifanya halmashauri kuanza na utekelezaji wa miradi mikubwa miwili ambayo ni ya ujenzi wa kituo  cha kisasa cha mabasi ya kubeba abiria, pamoja na ujenzi wa soko kubwa ambalo litasaidia kuongeza mapato na kutoa ajira kwa wananchi wa wilaya hiyo.

No comments: