Tuesday, March 15, 2016

MAJAMBAZI TUNDURU YAUA MWENYEKITI KWA RISASI NA KUPORA FEDHA



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WATU wanaodaiwa kuwa ni majambazi, wamemuua kwa kumpiga risasi Mwenyekiti wa kitongoji cha Chilundundu, Zubery Mohamed (53) na kufanikiwa kumpora kiasi cha shilingi 80,000.

Sambamba na mauaji hayo, pia majambazi hao walipiga risasi nne hewani na kufanikiwa kupora kiasi cha shilingi 470,000 mali ya Mkalela Muhidin (28) tukio ambalo lilifanyika, majira ya usiku.

Zubery Mwombeji.
Tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia Marchi 11mwaka huu, katika kitongoji hicho kijiji  cha Misechela wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma.

Baadhi ya mashuhuda walisema kwamba, katika matukio yote majambazi hao walitumia bunduki aina ya SMG na kwamba katika tukio la kwanza lililotokea kwenye kitongoji cha Mkalela kijiji cha Misechela, maharamia hao walifyatua hewani risasi na kufanya uporaji huo wa shilingi 470,000. 

Walisema katika tukio la pili maharamia hao, walimpiga risasi nne na kumuua Mohamed wakati akiwa anatumia upanga ili kuweza kupambana na majambazi hao, majira hayo ya usiku.


Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Zubery Mwombeji amethibitisha kuwepo kwa matukio hayo na kwamba tayari kuna watu watatu wanashikiliwa ambao wanadaiwa kuhusika na mauaji hayo, na majina yao yamehifadhiwa kwa sababu za kiusalama kutokana na uchunguzi bado unaendelea kuhusiana na matukio hayo.

 Alisema katika kuhakikisha kuwa wanakamilisha kazi hiyo kwa haraka, tayari amekwisha tuma viongozi waandamizi wa jeshi la Polisi kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa kina, ili kubaini ukweli uliopo juu ya matukio hayo.

Alisema ametoa maelekezo kwa jeshi la Polisi wilayani Tunduru, kuendesha msako mkali ili kuweza kuwanasa  watuhumiwa hao na kujiridhisha juu ya mambo hayo, yanayohatarisha usalama wa watu na mali zao.

Kamanda Mwombeji ametoa wito pia kwa wananchi, wenye taarifa zitakazofanikisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao kwa lengo la kulisaidia jeshi hilo, ili liweze kuwakamata kabla ya kuleta madhara kwa watu wengine.

Mganga aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu Mohamed, Dkt. Titus Tumbu alisema kuwa chanzo cha kifo hicho kilisababishwa kutokwa na damu nyingi baada ya risasi hizo kupenya kutoka upande wa bega la kulia, yaani kifuani na kutokeza upande wa nyuma kati kati ya mgongo wake.

No comments: