Sunday, March 6, 2016

NAIBU WAZIRI WA UJENZI ATOA AMRI YA KUBOMOLEWA KWA KITUO CHA MAFUTA TUNDURU


Na Steven Augustino,
Tunduru.

NAIBU Waziri wa ujenzi, uchukuzi na mawasiliano Mhandisi Edwin Ngonyani, ameamuru kuvunjwa mara moja kituo cha kuuza mafuta cha kampuni ya Cross roads, ambacho kinamilikiwa na Saleh Ahamad mjini Tunduru mkoani Ruvuma, ili kupisha ujenzi wa barabara inayojengwa kwa kiwango cha lami.

Aidha Waziri huyo pia amemwagiza Katibu tawala wa wilaya hiyo, Ghaib Lingo kushirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani Tunduru, kufanya uchunguzi juu ya uhalali uliotumika kumpatia kibali cha kujenga kituo hicho katika eneo ambalo sio rasmi.

Kwa mujibu wa maagizo hayo, Ngonyani ameagiza hatua kali zichukuliwe kwa wahusika wote ikiwa ni pamoja na kuwataka kumlipa fidia ya hasara atakayoipata, kutokana na zoezi hilo la uvunjaji litakapofanyika. 


“Haiwezekani serikali ibebe mzigo kutokana na uzembe wa watu wengine, kuruhusu kujenga vituo vya mafuta katika maeneo ambayo siyo rasmi na barabara inatakiwa ipite", alisema Ngonyani.

Ngonyani alitoa maagizo hayo wakati alipofanya ziara ya kikazi hapa mkoani Ruvuma, iliyoambatana na ukaguzi wa ujenzi wa barabara inayoendelea kujengwa kwa kiwango cha lami kutoka Songea kwenda Tunduru na Tunduru kuelekea Masasi, ikiwani ni juhudi ya serikali kutaka kufungua mikoa ya Kusini ipitike kwa urahisi.

Akizungumza kwa nyakati tofauti na wakandarasi wanaojenga barabara hiyo, Meneja wa wakala wa barabara (TANROADS) mkoa humo, Mhandisi Mathew Mtegumle aliwataka wakandarasi hao kuongeza bidii katika ujenzi huo na kuhakikisha kwamba, barabara hiyo inakamilika kwa wakati.

Naye Katibu tawala wa wilaya ya Tunduru, Ghaib Lingo pamoja na kuyapokea maelekezo hayo aliahidi kufuatilia, kuyasimamia na kuhakikisha zoezi hilo linatekelezwa kwa wakati.

No comments: