Friday, March 25, 2016

UWT RUVUMA YAMPONGEZA MAGUFULI UTENDAJI WAKE WA KAZI




Na Kassian Nyandindi,
Songea.

JUMUIYA ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) mkoani Ruvuma, imempongeza Rais John Magufuli kwa kazi anazozifanya za utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kitendo ambacho kimeelezwa kuwa kufanya hivyo ni kujenga imani kwa wananchi na serikali yao.

Pongezi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa UWT mkoani humo, Kuruthumu Mhagama alipokuwa kwenye kikao cha baraza maalumu la jumuiya hiyo kilichofanyika mjini hapa, mwishoni mwa wiki iliyopita.

Kuruthumu alisema serikali ya awamu ya tano, chini ya kauli mbiu ya Hapa kazi tu imedhamiria kuwaletea maendeleo ya kweli wananchi wake na kwamba kinachotakiwa sasa, kila mwananchi ahakikishe anatekeleza majukumu yake ipasavyo kwenye eneo lake ili dhamira ya serikali kuwaletea maendeleo iweze kutimia.


Mhagama alisema kuwa pia uamuzi wa Rais kumchagua makamu wake, Samia Suluhu Hassan lilikuwa ni jambo jema ambalo limeendelea kuwapa msukumo mkubwa wanawake, hasa ikizingatiwa kuwa tangu nchi ipate uhuru mwaka 1961 hajawahi kuchaguliwa mwanamke kuongoza nafasi hiyo.

“Nachukua nafasi hii kwa niaba ya wanachama wote wa UWT mkoani hapa, kuwapongeza na kuwashukuru wanachama wote wa CCM kwa kumpigia kura za ndio Rais Magufuli, lakini pia ni muhimu sisi kama wanawake tumshukuru kwa uamuzi wake wa kumteua makamu wa rais mwanamke”, alisema Kuruthumu.

Kuruthumu alisema kwamba Umoja huo wa wanawake hapa Ruvuma umedhamiria kuendelea kuhamasisha wanawake, ambao sio wanachama wa jumuiya hiyo wajiunge sambamba na kutekeleza umuhimu wa kulipa ada zao za uanachama kwa wakati.

Alisema madiwani wa viti maalumu naom wanapaswa kutekeleza majukumu yao ya utekelezaji wa ahadi zao, ambazo walizitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita, ili wananchi waweze kujenga imani nao ikiwemo chama na serikali kwa ujumla.

Hata hivyo alitahadharisha juu ya wanachama wenye tabia ya kukisaliti chama wakati wa chaguzi mbalimbali, kitendo ambacho katika uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka jana kulijitokeza katika baadhi ya maeneo, kupoteza kata na majimbo.

No comments: