Thursday, June 15, 2017

BREAKING NEWS: AFISA MAENDELEO YA JAMII WILAYA SONGEA AFUKUZWA KAZI KWA MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA SERIKALI

Na Mwandishi wetu,       
Songea.

BARAZA la Madiwani Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, limemfukuza kazi Afisa maendeleo ya jamii wa wilaya hiyo, Wenisalia Swai kutokana na kubadili matumizi ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Ofisi ya halmashauri hiyo bila kufuata taratibu husika.

Aidha Swai anadaiwa kutenda kosa la kubadili fedha shilingi milioni 130 zilizotolewa na ubalozi wa Japan hapa nchini, kwa ajili ya kuboresha kituo cha afya Mhukuru kilichopo wilayani humo kwa kumlipa mkandarasi aliyejenga jengo la halmashauri katika kijiji cha Lundusi kata ya Maposeni, wakati fedha kwa ajili ya ujenzi huo zilikwishatolewa na serikali.

Pia mtumishi huyo imeelezwa kuwa alibadili matumizi ya fedha nyingine zaidi ya shilingi milioni 156 zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa Skimu ya umwagiliaji katika kijiji cha Nakahuga na kuzielekeza kwenye utengenezaji wa madawati na ujenzi wa jengo la maabara, jambo ambalo limesababisha wakulima wa kijiji hicho kushindwa kuendesha na kunufaika na mradi huo wa umwagiliaji.


Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Songea, Simon Bulenganija alisema kuwa, Swai alipokuwa Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kabla ya Rais Dkt. John Magufuli hajateua wakurugenzi wa halmashauri za wilaya, miji, manispaa na majiji mwaka jana kwa kushirikiana na baadhi ya watumishi wengine akiwemo Mweka hazina wa halmashauri hiyo, Mwajuma Sekelela na Mkuu wa kitengo cha manunuzi Amina Njogela walibadili matumizi ya fedha hizo bila kupata idhini ya Kamati husika ya fedha, mipango na uchumi.

Akizungumza na mwandishi wetu jana Ofisini kwake mara baada ya kumalizika kwa baraza maalumu la kinidhamu, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Bulenganija alieleza kuwa awali watumishi hao wote watatu tayari walikwisha simamishwa kazi miezi minne iliyopita kwa lengo la kupisha uchunguzi kutokana na tuhuma hizo, hasa baada ya kubainika kwamba walichukua maamuzi ya kutumia fedha hizo kama mali yao binafsi.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa mbali na kufukuzwa kazi Afisa maendeleo huyo, baraza hilo kwa pamoja limekubaliana kumshusha cheo Mweka hazina wa halmashauri, Mwajuma Sekelela baada ya kupatikana na kosa la kushiriki na kupitisha ubadilishaji wa  matumizi ya fedha hizo hatua ambayo ilisababisha madiwani hao kuwa na mashaka naye.

Kadhalika baraza hilo limemrudisha kazini Mkuu wa kitengo cha manunuzi, Amina Njogela ambaye naye alisimamishwa kazi na wenzake kwa kosa la kushiriki katika maamuzi ya kubadilisha matumizi ya fedha hizo na kuchelewesha mchakato wa ujenzi wa Skimu hiyo ya umwagiliaji kijiji cha Nakahuga.


Hata hivyo Bulenganija alitoa wito kwa watumishi wengine wa halmashauri ya wilaya ya Songea kuwa waadilifu na waaminifu katika majukumu yao ya kazi za kiutumishi kila siku kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

No comments: