Saturday, June 17, 2017

RUHUWIKO SONGEA WAONDOKANA NA KERO YA MAJI SAFI NA SALAMA

Na Muhidin Amri,    
Songea.

WAKAZI wanaoishi katika mtaa wa Ruhuwiko Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wameondokana na kero ya muda mrefu ya upatikanaji wa maji safi na salama baada ya kukamilika kwa mradi mkubwa wa ujenzi wa tanki la maji katika mtaa huo ambalo sasa husambaza maji hayo katika maeneo mbalimbali wanayoishi.

Abdul Mshaweji.
Aidha katika hatua nyingine wametakiwa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na serikali hii ya awamu ya tano katika kumaliza kero wanazokabilianazo wananchi wake.

Sambamba na hilo wamekumbushwa pia wajibu wao wa kuisaidia serikali juu ya mkakati wa kuinua uchumi wao kwa kubuni miradi ya maendeleo ambayo itawaingizia kipato kuanzia ngazi ya familia.

Meya wa Manispaa ya Songea, Abdul Mshaweji alitoa kauli hiyo jana wakati alipokuwa akizungumza na wakazi wa mtaa huo, katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na wananchi hao wakilenga kuishukuru serikali kwa kukamilisha ujenzi wa mradi huo wa maji katika mtaa huo wa Ruhuwiko.


Mshaweji alisema kuwa ameiagiza kamati inayosimamia mradi huo kuhakikisha kwamba inajiepusha na vitendo vya upendeleo katika kuendesha mradi huo badala yake wahakikishe kwamba, kila mwananchi anachangia na kulipia bili za matumizi ya maji kila mwishoni mwa mwezi ili uweze kuwa endelevu na kuwezesha kupatikana fedha kwa ajili ya kuufanyia matengenezo hasa pale linapotokea tatizo la kuharibika mabomba ya kutolea maji.

“Natambua matatizo ya baadhi ya wananchi kutokuwa na mwamko wa uchangiaji fedha katika huduma mbalimbali za kijamii, lakini nawasihi wakazi wa eneo hili muwe mfano wa kuigwa kwa kuchangia huduma hii ili iweze kuwa endelevu”, alisisitiza Mshaweji.

Pamoja na mambo mengine kwa nyakati tofauti wananchi wa mtaa wa Ruhuwiko walipozungumza na mwandishi wetu, walisema kuwa wanatambua mchango huo uliotolewa na serikali kwamba imetumia fedha nyingi katika ujenzi wa mradi huo hivyo wanaishukuru na kwamba wataendelea kutekeleza kwa vitendo yale yote ambayo wanapaswa kuyatekeleza katika kuuendeleza mradi huo wa maji.

No comments: