Wednesday, June 28, 2017

WAUMINI WA KIISLAMU WATAKIWA KUJIEPUSHA NA MAMBO YANAYOKWENDA KINYUME NA MAFUNDISHO YA DINI YAO

Baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu mtaa wa Making’inda Manispaa ya Songea wakifuatilia nasaha kutoka kwa Imamu wa Msikiti wa Making’inda Shehe Bashiru Matembo (hayupo pichani) wakati wa swala ya Ed el Fitri jana ambapo waumini hao waliaswa kuendeleza mambo mema waliyokuwa wakifanya wakati wa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Waumini wa Kiislamu kutoka mtaa wa Making’inda Manispaa ya Songea, wakitoka nje baada ya kuswali swala ya Ed el Fitri.
Na Muhidin Amri,    
Songea.

IKIWA ni siku chache zimepita katika kusherehekea sikukuu ya Idd el Fitri, Waislamu hapa nchini wametakiwa kujiepusha na mambo  yanayokwenda kinyume na mafundisho ya dini yao, ikiwemo matendo ya uzinzi na tabia ya  kujengeana fitina badala yake wanapaswa kuendelea kutenda mambo  mema waliyokuwa wakiyafanya wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Aidha wameombwa kudumisha upendo, undugu na mshikamano miongoni mwao na hata kwa watu wasiokuwa Waislamu hatua ambayo itasaidia kuwa na jamii ya watu wastaarabu ambao wakati wote wataishi na kumcha Mungu.

Imamu wa Msikiti wa Making’inda kata ya Msamala Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, Shehe Bashiru Yahay Matembo alisema hayo jana wakati akitoa nasaha kwa waumini wa kiislamu huku akisisitiza kuwa Waislamu wanapaswa kutumia sikukuu ya Idd el Fitri, kwa ajili ya kusameheana na kuomba msamaha kwa yule aliyemkosea  badala ya kuendeleza chuki na uhasama kati yao.


Alisema kuwa wakati umefika sasa kwa Waislamu pia kuwa kitu kimoja na kuendeleza utamaduni wa undugu pamoja na kukataa mambo mabaya kwa kuhimizana kutenda mambo mazuri, kwani kufanya hivyo husaidia kudumisha mshikamano uliokuwepo hapo awali.

Kwa mujibu wa Shehe Matembo alieleza kuwa kwa waumini wa dini hiyo kurudia tena kufanya maovu haipendezi na kwamba kumalizika kwa mwezi mtukufu wa Ramadhani, iwe ndiyo mwanzo wa kuongeza  jitihada katika kutenda na kufuata mambo mema ikiwemo kusoma kitabu kitukufu cha Quran, hatua ambayo itawasaidia hata katika kufahamu vizuri dini yao pamoja na kuzidisha upendo miongoni mwao.


Pia amewakumbusha wazazi wahakikishe kwamba wanawatunza na kuwalea watoto wao katika misingi ya dini, ili kuepukana na kizazi kisichomjua Mungu jambo ambalo ni hatari kwa kuwa jamii isiyomcha Mwenyezi Mungu ndiyo chanzo cha kuongezeka na kukithiri kwa vitendo vya uzinzi, ulevi na wizi wa mali za umma.

No comments: