Friday, June 16, 2017

WAZIRI TAMISEMI AWAONYA WAKUU WA MIKOA NA WILAYA

WAZIRI wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene amewaonya Wakuu wa mikoa na wilaya, ambao wanatumia vibaya madaraka yao ya kukamata watu walio kwenye himaya zao.

Alitoa onyo hilo leo wakati alipojibu maswali ya wabunge waliotaka kufanyika marekebisho ya sheria inayowapa mamlaka wakuu hao ya kuwakamata na kuwaweka ndani wananchi wanaowatuhumu kwa lolote.

Licha ya kubainisha kwamba sheria hiyo haina tatizo, Waziri huyo amesisitiza kwamba, ukamataji unatakiwa ufanywe kwa mtu aliyetenda kosa la jinai au anayehatarisha usalama, “isiwe kwa show-off tu”, alisema.


Vilevile aliongeza kuwa mhusika anayekamatwa na kuwekwa ndani anatakiwa kufikishwa Mahakamani mara moja na asishikiliwe tu.

Alisisitiza kuwa wakuu hao wa mikoa na wilaya ni wawakilishi wa Serikali kwenye maeneo yao, hivyo hawatakiwi kutumia vibaya madaraka waliyokasimiwa.


Katika siku za hivi karibuni wakuu wa mikoa na wilaya wamekuwa wakilalamikiwa kuwaweka watu kizuizini pasipo kuwa na sababu za msingi, miongoni mwao wakiwamo waandishi wa habari.

No comments: