Monday, June 12, 2017

HALMASHAURI WILAYA YA SONGEA YAJIVUNIA KUFIKISHA HUDUMA YA MAJI KATIKA MAKAZI YA WANANCHI WAKE

Na Muhidin Amri,     
Songea.

JUMLA ya shilingi milioni 65.710 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa kisima cha maji  katika kijiji cha Lundusi kata ya Maposeni, Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma ikiwa ni malengo ya kufikisha huduma  ya maji safi na salama katika makazi ya wananchi wanaoishi kwenye maeneo ya kijiji hicho.

Mhandisi wa maji wa halmashauri hiyo Isaac Nyirenda alisema kuwa mbali na wananchi hao kufikishiwa katika makazi yao pia maji hayo yatapelekwa makao makuu ya halmashauri pamoja na nyumba ya kuishi Mkurugenzi mtendaji na watumishi wengine wa halmashauri.

Alisema kuwa mpango wa baadaye ni kuhakikisha kwamba huduma hiyo inawafikia wananchi wengi zaidi ambao wanaishi katika maeneo mbalimbali ya kata yote ya Maposeni na kata nyingine za jirani.


Kwa mujibu wa Mhandisi huyo alifafanua kuwa kazi zote za ujenzi huo wa kisima zimefanywa kwa kutumia mafundi na wataalamu wa halmashauri kwa kushirikiana na mafundi wadogo ambao waliingia nao mikataba.

Nyirenda alieleza kuwa hadi sasa kazi iliyofanyika ni uchimbaji visima vitatu na matanki yake ya kuhifadhia maji, ujenzi wa nyumba ya kuishi mlinzi pamoja na uzio, uchimbaji wa choo na mtaro kilometa 1.145, ununuzi wa mabomba na viunganishi vyake pamoja na ununuzi wa pampu tatu za kuvuta maji.

Alibainisha kuwa Pampu iliyofungwa katika kisima hicho ni ya aina ya “Grundfos Pump” yenye uwezo wa nguvu kiasi cha kilowati 1.5 ambayo uwezo wake ni mkubwa wa kusukuma maji kwa mita 150.


Pia kwenye matanki hayo ya hifadhi ya maji itakuwa na uwezo wa kusukuma maji kwa kiwango cha lita 8,400 kwa saa au lita 140 kwa dakika na visima hivyo vina ujazo wa mita za ujazo 13.73 ambazo ni sawa na lita 13, 730 kwa wakati mmoja.

No comments: