Friday, June 16, 2017

MADABA WATAKIWA KUONGEZA UZALISHAJI WA MAZAO SHAMBANI

Na Muhidin Amri,    
Madaba.

WAKULIMA katika Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma wametakiwa kuchangamkia fursa na mkakati uliowekwa na serikali ambao unataka nchi kufikia katika uchumi wa kati, kupitia ujenzi wa viwanda vya aina mbalimbali ifikapo mwaka 2020 hadi 2025.
Shafi Mpenda.

Vilevile katika kufanikisha hilo imeelezwa kuwa wanapaswa kuongeza uzalishaji wa mazao mashambani ili viwanda hivyo vitakapoanzishwa, viweze kusonga mbele na kusaidia kuongeza thamani ya ubora wa mazao hayo.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Shafi Mpenda alisema hayo juzi wakati alipokuwa akikagua mradi wa shamba la mahindi la vijana, ambao hujishughulisha pia na uendeshaji wa Pikipiki maarufu kwa jina la Boda boda katika kijiji cha Lutukira wilayani humo ili waweze kujipatia kipato.


Alisema kuwa wilaya ya Madaba ni maarufu kwa uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara kutokana na uwepo wa hali nzuri ya hewa, lakini bado wananchi wake wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha kutokana na mazao wanayolima hayawanufaishi ipasavyo kwa sababu ya ukosefu wa soko la kuuzia mazao hayo na viwanda vya kusindika ambavyo vingewawezesha kuongeza thamani ya mazao yao.


Mpenda aliongeza kuwa wakulima hao licha ya juhudi kubwa wanazozifanya mwaka hadi mwaka katika kuzalisha mazao ya tangawizi, matunda ya aina mbalimbali, mahindi na mpunga bado changamoto wanayokabiliana nayo ni soko la uhakika na viwanda vitakavyoweza kuongeza thamani ya mazao hayo wanayozalisha.


“Halmashauri hii ya Madaba ina utajiri mkubwa wa ardhi na rasilimali watu na kwamba tutaweza kupiga hatua mbele kiuchumi endapo tu wananchi hawa hasa kwa upande wa wakulima, wataweza kubadili mfumo kutoka kilimo cha mazoea (zamani) na kuingia katika mfumo wa kisasa kwa kutumia kilimo cha Trekta na kuweka shambani pembejeo bora za kisasa kipindi cha upandaji wa mazao yao”, alisema.

No comments: