Monday, September 4, 2017

BENKI YA DUNIA YAFADHILI UBORESHAJI WA BUSTANI MANISPAA YA SONGEA

Uboreshaji wa Manispaa ya Songea ukiendelea kufanyika.
Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

IMEELEZWA kuwa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma imepokea jumla ya shilingi milioni 400 kwa ajili ya uboreshaji wa bustani ya Manispaa hiyo.

Mradi huo unafadhiliwa na Benki ya dunia chini ya Mpango wa Kuzijengea Uwezo Serikali za Mitaa (ULGSP) na kwamba unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 399.95.

Hayo yalisemwa na Afisa habari wa Manispaa ya Songea, Albano Midelo wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu mjini hapa ambapo alifafanua kuwa fedha ambazo zimekwisha lipwa hadi sasa ni shilingi milioni 97.83 na fedha iliyobaki ni shilingi milioni 302.12.


Alisema kuwa mradi huo unatekelezwa kwa ujenzi wa miundombinu mbalimbali katika kipindi cha miezi sita ambapo ulianza kujengwa Machi 15 mwaka huu na unatarajiwa kumalizika ujenzi huo Septemba 30 mwaka huu.

Mradi huo ambao upo mkabala na Ofisi za halmashauri ya Manispaa hiyo unajengwa eneo la mgahawa, choo cha kulipia, uzio na maeneo ya kupaki magari (Parking bay).

Pia aliongeza kuwa bustani hiyo katika mji wa Songea ina eneo la kupumzikia (Resting huts) na kwamba hatua ya ujenzi imefikia zaidi ya asilimia 70.

Maeneo mengine ambayo yanaendelea katika bustani hiyo ni ujenzi wa uzio kuzunguka bustani yote, utengenezaji wa bustani ambayo inawekwa udongo na kupandwa nyasi na miti na ujenzi wa mnara na kazi ya kusambaza maji katika eneo la ujenzi.

Manispaa ya Songea ni moja kati ya halmashauri za miji na Manispaa 18 za Tanzania bara ambazo zipo katika mpango wa ULGSP ikiwa ni lengo la kuendeleza miundombinu yake.


No comments: