Tuesday, September 5, 2017

DC SONGEA AWASHITAKI TANESCO KWA RAIS DOKTA MAGUFULI

Na Kassian Nyandindi,   
Songea.

MKUU wa  Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Pololet Mgema amewashushia lawama na kuwashitaki kwa Rais Dokta John Pombe Magufuli wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) mkoani humo kwamba wanafanya kazi  kwa mazoea, badala ya kwenda na kasi ya awamu ya tano inayolenga kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa mpango wa kuharakisha maendeleo hapa nchini.
Mkuu wa wilaya ya Songea, Pololet Mgema.

Mgema alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati akizungumza na wananchi na baadhi ya wafanyakazi wa Shirika hilo katika kijiji cha Litapaswi kata ya Mpitimbi wilayani humo.

Kwa mujibu wa Mgema alisema kuwa wafanyakazi hao wameshindwa kubadilika na kuendana na kasi ya Rais Dokta Magufuli kwa kile alichoeleza kuwa wamekuwa wakitumia muda mwingi kukaa ofisini na kusubiri wateja badala ya kuwafuata walipo jambo ambalo linasababisha baadhi ya watu kutofikishiwa huduma ya umeme kwa wakati.


“Bado watumishi wa TANESCO wanafanya kazi kwa mazoea kwa kuwasubiri wateja ofisini badala ya kuwafuata pale walipo, kuna wateja wakubwa wanahitaji huduma ya umeme kwa ajili ya shughuli zao lakini watumishi hawa ni kikwazo kikubwa, wanatumia muda mwingi kukaa ofisini badala ya kwenda kwa mteja”, alisema Mgema.

Aidha Mkuu huyo wa wilaya aliishukuru serikali ya awamu ya tano kwa kuhakikisha mkoa wa Ruvuma unaunganishwa na gridi ya taifa chini ya mradi wa Makambako Songea ambao unatarajia kukamilika mwakani.

Alisema kuwa serikali ya mkoa huo itahakikisha inakuwa karibu na kufuatilia ujenzi wa mradi huo ili uweze kukamilika kwa wakati na kuwawezesha wananchi kuharakisha kukua kiuchumi kupitia nishati ya umeme.

Mkoa wa Ruvuma una vijiji 507 hata hivyo vijiji vitakavyo bahatika kuunganishiwa umeme ni 209 ambapo ameiomba serikali chini ya Wizara ya nishati kuhakikisha kwamba vijiji vilivyobakia vinaingizwa katika mpango huo wa kupata umeme.


Hata hivyo Mgema aliongeza kuwa umeme huo utaweza kuchochea kukua kwa uchumi wao kwa kuanzisha viwanda vidogo vidogo na vikubwa, hasa ikizingatiwa kuwa zaidi ya asilimia 80 ya wakazi wake wanategemea kilimo hivyo umeme utasaidia kuanzisha viwanda kwa ajili ya kuongeza thamani mazao mbalimbali wanayozalisha.

No comments: