Friday, September 15, 2017

UHONDE AWATAKA WANACCM SONGEA KUVUNJA MAKUNDI

Na Dustan Ndunguru,      
Songea.

KATIBU wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Rajab Uhonde amewataka wanachama wa chama hicho wilayani humo kuvunja makundi yote yaliyokuwepo wakati wa mchakato wa kuwapata viongozi wa chama kuanzia ngazi ya shina, matawi na kata ili kuweza kuendelea kujenga ushindi katika chaguzi zijazo za dola.

Uhonde alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake, kuhusiana na jinsi ambavyo chama hicho kilivyoweza kufanikisha kukamilisha chaguzi mbalimbali kwa ngazi hizo.

Alisema kuwa baada ya kukamilika kwa chaguzi hizo na kufanikiwa kuwapata viongozi ndani ya chama kinachotakiwa sasa ni kwa wanachama kubaki wamoja na pale ambapo patajitokeza kasoro vikao halali vitumike kumaliza kasoro hizo na sio vinginevyo.


Alifafanua kuwa CCM hivi sasa inajipanga kufanya uchaguzi kwa ngazi ya wilaya na kwamba aliwaasa viongozi wote waliokwisha chaguliwa wajipange kikamilifu ikiwemo kufanya vikao vilivyo kwa mujibu wa katiba ya chama ili kufanikisha masuala muhimu ambayo yataweza kuleta ufanisi.

Alisema lengo la chama chochote cha siasa ni kushika dola hivyo ili hilo liweze kutimia ni muhimu kwa wanachama kuacha migongano miongoni mwao na kwamba wanapaswa kushirikiana ambapo kwa kufanya hivyo ushindi utapatikana bila shaka katika uchaguzi ujao wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu.


Kuhusu wanachama wenye tabia ya kuhama chama baada ya kushindwa kwenye uchaguzi ndani ya chama alisema huu ni uroho wa madaraka, badala yake wanapaswa kufahamu kwamba katika uchaguzi wa aina yoyote ile kunakuwa na matokeo mawili kushinda au kushindwa, hivyo pindi inapotokea kushindwa wanapaswa kuvuta subira na kuwa wavumilivu hadi chaguzi zingine na sio kukimbilia vyama vya upinzani.

No comments: