Friday, September 15, 2017

WANUFAIKA WA TASAF MBINGA WATAKIWA KUWA NA MATUMIZI MAZURI YA FEDHA WANAZOPATA

Na Dustan Ndunguru,    
Mbinga.

WANUFAIKA waliopo katika mpango wa kunusuru kaya maskini, ambao unasimamiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kutumia vizuri fedha wanazozipata kutoka kwenye mfuko huo kwa kuanzisha miradi midogomidogo ambayo itawakwamua kiuchumi.

Emmanuel Fikiri ambaye ni Afisa ufutiliaji wa TASAF wilayani humo, alisema hayo juzi wakati alipokuwa akizungumza na wanufaika wa kijiji cha Mihango mara baada ya kutembelea na kukagua miradi yao ya ufugaji ambayo wameianzisha kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita.

Alisema kuwa malengo ya mpango huo wa kunusuru kaya maskini ni kuweza kuwainua kiuchumi wananchi ambao hali zao kimaisha ni duni sio za kuridhisha.


Fikiri alieleza kuwa miradi midogomidogo ya ufugaji kama vile wa kuku wa kienyeji ni mzuri kwani ufuatiliaji wake ni rahisi, kutokana na ukweli kwamba kuku hao hawashambuliwi kwa urahisi na magonjwa na mfugaji huweza kupata mafanikio makubwa kwa muda mfupi.

“Nimewatembelea wanufaika ambao wamejikita na ufugaji wa kuku na nguruwe kweli nafarijika na kazi wanazozifanya, niwaombe tu waendelee kutumia vyema fedha wanazozipata na wajiepushe na matumizi mabaya ikiwemo kuendekeza unywaji wa pombe”, alisema Fikiri.

Afisa ufuatiliaji huyo alisema ofisi yake itaendelea kufuatilia kwa karibu matumizi ya fedha hizo zinazotolewa na mfuko huo, kwa lengo la kuweza kunusuru kaya maskini wilayani humo na kwamba viongozi wa vijiji na kata wanapaswa kupitia mikutano yao ya hadhara wahakikishe wanaendelea kuhamasisha na kuwaelimisha wale ambao ni walengwa wa mpango huo juu ya matumizi bora ya fedha hizo ili waweze kuendelea kuimarisha miradi yao midogo wanayoianzisha hatimaye waondokane na umaskini.


Fikiri alisisitiza pia juu ya umuhimu wa wanufaika hao kujiunga na mfuko wa bima ya afya ili hatimaye waweze kunufaika na matibabu bure kwa kipindi cha mwaka mzima na kwamba fedha wanazozipata.

No comments: