Thursday, September 7, 2017

MANISPAA SONGEA YAGAWA VYANDARUA KWA WANAFUNZI NA WAZEE

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Songea, Abdul Mshaweji akiwa katika zoezi la ugawaji wa vyandarua katika mitaa mbalimbali ya Manispaa hiyo mjini hapa.
Na Kassian Nyandindi,    
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imegawa vyandarua 35,874 kwa wanafunzi wa shule za msingi 81 zilizopo katika Manispaa hiyo ili kuweza kukabiliana na ugonjwa wa Malaria.

Katika Manispaa hiyo pia imegawa vyandarua 450 kwa wazee wasiokuwa na uwezo katika mitaa mbalimbali iliyopo mjini hapa ambapo zoezi hilo pia malengo yake ni kufikia hatua ya kuwagawia vyandarua 1,000.

Albano Midelo ambaye ni Afisa habari wa Manispaa hiyo, alisema hayo leo wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu huku akiongeza kuwa hizo ni jitihada za kuutokomeza ugonjwa wa Malaria.


Midelo alifafanua kuwa halmashauri hiyo pia imepokea lita 1,000 za dawa ya kuua Mbu wanaoeneza ugonjwa huo na kwamba muongozo wa namna ya kutumia dawa hiyo, umekwisha tolewa na serikali mwishoni mwa mwezi Julai mwaka huu huku zoezi la upuliziaji kwenye maeneo mbalimbali linatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa.

Kiwango cha maambukizi ya Malaria katika halmashauri ya Manispaa ya Songea ni asilimia 2.5.

Alibainisha kuwa hatua ambazo zinachukuliwa na Manispaa hiyo katika kupambana na ugonjwa huo ni pamoja na kuhakikisha kwamba upatikanaji wa dawa na vitenganishi kwa ajili ya matibabu vinakuwa vya kutosha ikiwemo na utekelezaji mradi mdogo wa kitaifa wa usambazaji vyandarua kwa wanafunzi shule za msingi.


Mikakati mingine ya kupambana nao ni kuendelea kuhamasisha na kuelimisha jamii juu ya matumizi sahihi ya vyandarua, kufanya zoezi la utambuzi wa mazalia ya mbu kwenye kata zote ambazo zina maambukizi makubwa ya malaria hayo ikiwemo na ufuatiliaji wa tiba sahihi ya ugonjwa huo.

No comments: