Friday, September 1, 2017

DC MBINGA AKEMEA WAFUGAJI WASIOPELEKA WATOTO SHULE AWATAKA KUFUATA TARATIBU NA MAELEKEZO YALIYOWEKWA NA SERIKALI

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye akihutubia wananchi na wafugaji (hawapo pichani) siku ya zoezi la uzinduzi upigaji chapa mifugo (Ng'ombe) katika kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani Mbinga ambapo aliwataka wafugaji hao kuzingatia maagizo na maelekezo yanayotolewa na serikali na kwamba kwa atakayekaidi atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Kikundi cha akina mama ngoma za asili kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani Mbinga wakitumbuiza siku ya uzinduzi wa zoezi la upigaji chapa mifugo (Ngo'mbe) wilayani humo.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

WAFUGAJI waliopo katika wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kupeleka watoto wao shule na kuacha tabia ya kuwafanya kuwa vibarua wa kuchunga mifugo.

Mkuu wa wilaya hiyo, Cosmas Nshenye alisema hayo juzi wakati alipokuwa mgeni rasmi akihutubia wananchi na wafugaji kwenye uzinduzi wa zoezi la upigaji chapa mifugo (Ng’ombe) katika kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani hapa.

“Hili sio ombi ni lazima, watoto wote wenye umri wa kwenda shule sharti wapelekeni shuleni ili waweze kuandikishwa waweze kusoma na kupata elimu itakayoweza kuwasaidia maishani mwao”, alisisitiza Nshenye.

Alisema kuwa ipo tabia watoto wa wafugaji wengi hawaendi shule na jambo hili linasababishwa na wazazi wao muda mwingi kuwatumikisha katika shughuli za kuchunga ngo’mbe badala ya kuwapeleka shule kwenda kusoma.


Vilevile katika hatua nyingine amewataka watendaji wa vijiji na kata kusimamia sheria namba 12 ya mwaka 2010 inayowataka wafugaji wote kusajili, kufanya utambuzi na ufuatiliaji wa mifugo yao ili kuweza kudhibiti tabia ya uingizaji holela wa mifugo na kusababisha migogoro baina ya wafugaji, wakulima na watu wa mipaka ya hifadhi na mazingira.

Hivyo katika utekelezaji wa zoezi hilo amezitaka halmashauri ya mji wa Mbinga na wilaya ya Mbinga zilizopo wilayani hapa kutekeleza agizo hilo la serikali kupiga chapa mifugo yote.

“Niwatake ndugu zangu wafugaji tuwe na mifugo michache lakini yenye tija kubwa aidha tuache kuchungia mifugo yetu kwenye mashamba yenye mazao au kuchungia kwenye misitu iliyohifadhiwa vyanzo vya maji atakayekiuka haya hatua kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa kwa wale wote watakaokaidi”, alisema.

Nshenye akizungumzia pia kuhusu upatikanaji wa malisho kwa ajili ya mifugo ya wafugaji wa wilaya hiyo alisema kuwa serikali inasisitiza mpango wa matumizi bora ya ardhi ambapo serikali za vijiji zinapaswa kutenga maeneo ya malisho ya mifugo kwa kuzingatia sheria ya ardhi namba 5 ya mwaka 1999 na sheria ya matumizi ya ardhi namba 6 ya mwaka 2007.

Awali akisoma taarifa ya idara ya mifugo na uvuvi, Mary Ndunguru ambaye ni afisa mifugo na uvuvi alisema kuwa zoezi hilo la upigaji chapa mwisho wake ni leo Septemba Mosi mwaka huu kwa halmashauri zote za mkoa wa Ruvuma.


Ndunguru alieleza kuwa kwa wilaya ya Mbinga zoezi hili lilianza Julai 24 mwaka huu kwa vijiji vyote 121 vilivyopo katika halmashauri ya wilaya ya Mbinga.

No comments: