Sunday, September 10, 2017

WAFURAHIA UTARATIBU WA UNUNUZI WA MAHINDI KATIKA VITUO VYA NFRA

Na Muhidin Amri,         
Songea.

BAADHI ya wakulima wa mahindi wilayani Songea mkoa wa Ruvuma wameipongeza serikali kwa  kuweka utaratibu mzuri juu ya suala la ununuzi wa mahindi na bei nzuri ambao umesaidia wakulima wengi kuuza mahindi yao kwa bei ya uhakika inayolingana na gharama ya uzalishaji.

Wakizungumza mbele ya Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge ambaye alitembelea vituo vya ununuzi wa zao hilo katika maeneo mbalimbali wilayani Songea walisema kuwa, utaratibu uliotumika kwa Wakala wa Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) kukunua mahindi kupitia vikundi umewezesha kazi hiyo kutoingiliwa na wajanja wachache ambao kila mwaka wamekuwa wakinunua mahindi ya wakulima kwa bei ndogo na wao kwenda kuuza NFRA kwa bei kubwa.

Walisema kuwa licha ya serikali kuweka mgawo mdogo wa mahindi kiasi cha tani 2,000 kwa halmashauri ya wilaya hiyo inayounda jimbo la Peramiho, utaratibu huo umewezesha kupunguza usumbufu kwa wakulima kukaa muda mrefu vituoni kusubiri kupimiwa mahindi yao tofauti na hivi sasa ambapo kila mkulima anatumia kikundi chake kwa kuuza tena kwa muda mfupi.


Batholomeo Nkwera  ambaye ni mwanachama wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ameipongeza serikali ya awamu ya tano kwa umakini  wake katika kushughulikia mahitaji na matatizo mbalimbali ya wakulima na kusisitiza kuwa, hatua hiyo itaendelea kuhamasisha wakulima kuongeza uzalishaji wa mazao.


Mkulima mwingine Athanas Komba aliongeza kuwa serikali imewatendea haki kwani licha ya kuweka mgao mdogo, hata hivyo umeepusha malalamiko na kuwapongeza wafanyakazi wa NFRA waliopo katika vituo vya ununuzi kwa kuwa wazi na utaratibu ambao kila mkulima ameridhika nao licha ya wengine kukosa nafasi ya kuuza mahindi yao.

No comments: