Saturday, September 16, 2017

WANANCHI WASHAURIWA KUEPUKA LUGHA ZA UPOTOSHAJI

Na Dustan Ndunguru,    
Mbinga.

WANANCHI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma wametakiwa kuepuka kusikiliza kauli za watu wanaopita kwenye maeneo yao wanayoishi, ambao hutoa lugha za upotoshaji kuhusiana na matumizi ya dawa zinazotolewa na serikali katika jamii kwa ajili ya kuzuia na kutibu magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele.

Kauli hiyo imetolewa jana na Mratibu wa magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele wa wilaya hiyo, Sebastian Mhagama wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi juu ya magonjwa hayo jinsi ambavyo yanavyoathiri jamii.

Mhagama alisema kuwa jitihada kubwa inaendelea kufanyika kila mwaka wilayani humo kutibu wale wote ambao huathirika sambamba na utoaji wa elimu kwa wananchi, ili kuwafahamisha namna ya kuepukana nayo lakini kikwazo kikubwa kimekuwa kutoka kwa baadhi ya watu ambao wamekuwa na tabia ya kuwakatisha tamaa wenzao wanaotumia dawa hizo.


Aliyataja magonjwa hayo kuwa ni usubi, kichocho, matende na mabusha ambayo licha ya kutopewa kipaumbele lakini hivi sasa yanapewa kipaumbele kikubwa na yamekuwa yanatibika na kuzuilika, hivyo serikali kupitia Wizara ya afya na ustawi wa jamii kwa kuhusisha halmashauri za wilaya dawa za magonjwa hayo zimekuwa zikitolewa kwa wananchi wote bila ubaguzi.

Alisema kuwa pamoja na magonjwa hayo kutopewa kipaumbele kwa siku za nyuma lakini bado yalikuwa na athari kubwa katika jamii na kwamba maeneo yaliyoathirika zaidi wilayani hapa ni ukanda wa bonde la ziwa Nyasa ambalo limeathirika kwa kichocho, usubi, minyoo ya tumbo, mabusha na matende kutokana na madimbwi ya maji ambayo huzalisha mbu kwa wingi.

Mhagama alifafanua kuwa jamii imeelimishwa kuhusiana na madhara ya magonjwa hayo na kuwapa dawa za kutibu na kuzuia ambapo hupewa mara moja kwa mwaka na pia dawa hizo hutolewa bure.


Kadhalika alieleza kuwa magonjwa hayo licha ya kutopewa kipaumbele bado ni vyema jamii ikatambua wazi kwamba madhara yake ni makubwa hasa pale binadamu yanapompata, hivyo jamii inashauriwa mara kwa mara kusikiliza ushauri unaotolewa na wataalamu ili kuweza kuepukana nayo au kuyatokomeza kabisa.

No comments: