Monday, September 11, 2017

DC APONGEZA JUHUDI ZINAZOFANYWA NA JKT KATIKA KUKUZA UCHUMI WA NCHI

Na Mwandishi wetu,           
Songea.

MKUU wa Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Cosmas Nshenye amepongeza juhudi zinazofanywa na kikosi cha Jeshi la Kujenga Taifa cha 842 Mlale JKT kwa ubunifu wao wa miradi mbalimbali ya kiuchumi, inayolenga kupunguza baadhi ya kero zinazokikabili kikosi hicho bila kutegemea msaada wa serikali na wahisani wengine.

Cosmas Nshenye.
Nshenye alitoa pongezi hizo juzi wakati alipokuwa akifunga mafunzo ya awali ya kijeshi Operesheni Tanzania ya viwanda kwa vijana 1,710 kwa mujibu wa sheria ambao wamemaliza mafunzo yao ya miezi mitatu.

Aidha amewaagiza makamanda na askari wa kikosi hicho kuendelea na mipango thabiti itakayoweza kuharakisha maendeleo ya mkoa huo, ikiwemo ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao yanayolimwa kwa wingi katika kikosi hicho na mkoa wote kwa ujumla.

Kadhalika aliwataka vijana waliomaliza mafunzo kutumia mafunzo hayo kwa manufaa ya Watanzania na nchi kwa ujumla kwa kukubali kujitolea wakati wote watakapohitajika hasa katika shughuli za ulinzi.


Alisema kuwa ni matumaini ya Watanzania kuona vijana wanaopitia Jeshi la kujenga taifa wanakuwa mfano wa kuigwa kwa kuwa mstari wa mbele katika kupambana na vitendo vya rushwa, matishio ya kiusalama kwa nchi, madawa ya kulevya na mmomonyoko wa madili badala yake huwa wa kwanza katika kukemea maovu yanayofanywa na wachache wasiothamini amani tuliyonayo.

Alisema Jeshi la kujenga taifa linaowajibu mkubwa wa kuwakutanisha vijana kutoka maeneo mbalimbali ya nchi na kuwaweka pamoja na kuwafundisha masomo ikiwemo  mafunzo ya kijeshi, uraia na stadi za kazi ambapo amewapongeza wakufunzi wa vijana waliomaliza mafunzo hayo kwa kujitoa kwa moyo wa dhati kuwafundisha vijana hao  kwa kuhakikisha wanafikia kiwango kilichokusudiwa.


Nshenye aliongeza kuwa mfunzo hayo yanayo umuhimu mkubwa katika nchi yetu katika kuweza kujenga kizazi bora kitakachoweza kuliweka taifa letu katika misingi iliyokuwa imara kwa Nyanja zote za kiuchumi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni.

No comments: