Wednesday, October 21, 2015

AMTWANGA NA MCHI KICHWANI NA KUSABABISHA MAUAJI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MKAZI mmoja wa kitongoji cha Makombe kijiji cha Milonde kata ya Matemanga wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, Mohamed Mawazo (43) anashikiliwa na Polisi kwa tuhuma ya mauaji.

Taarifa za tukio hilo, zinasema kuwa  mtuhumiwa huyo anashikiliwa akidaiwa kumuua Zuberi Issa kutokana na kipigo alichokipata kutoka kwa mtuhumiwa huyo ambaye alimpiga kwa kutumia mchi wa kutwangia, kutokana na wivu wa kimapenzi.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Revocatus Malimi.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, mtuhumiwa huyo alifanya kosa hilo kwa kumtwanga nao kichwani kitendo ambacho kilimsababishia kufikwa na mauti.

Kaimu Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Revocatus Malimi alisema kuwa tukio hilo lilitokea usiku wa Oktoba 16 mwaka huu.

Alisema baada ya mtuhumiwa huyo kufanya shambulizi hilo, alikwenda kuripoti kwa Mwenyekiti wa kitongoji cha Makombe, Said Mussa huku akitamba kuwa tayari amekwisha mpiga mtu aliyekuwa anamtuhumu kwamba anatembea na mke wake, ambaye ni miongoni mwa wake zake watatu.


Baada ya kiongozi huyo kupewa taarifa hizo, alichukua jukumu la kwenda kufuatilia tukio hilo kwa kushirikiana na ndugu wa jirani na marehemu huyo ambapo walimkimbiza Hospitali ya Kanisa la Upendo wa Kristu Kiuma, ambako baadaye alifariki akiwa anapatiwa matibabu.

Alisema baada ya kifo hicho, Mwenyekiti huyo wa kitongoji alitoa taarifa Polisi ambapo jitihada za kumtafuta mtuhumiwa zilifanikiwa, ambaye awali alikuwa amekimbia lakini alikamatwa.

Kamanda huyo wa Polisi, amewaasa wananchi kuachana na tabia za kuchukua sheria mkononi, kwani kufanya hivyo ni kosa la jinai.

Mganga aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu, Zuberi Issa (36), Dokta Gaofrid Mvile alisema chanzo cha kifo hicho kilisababishwa na kuchanganyika kwa damu na ubongo, kulikosababishwa na  kupasuka kwa fuvu la kichwa chake.

Alisema katika tukio hilo marehemu, aliumia vibaya sehemu ya nyuma katika kichwa chake.

No comments: