Friday, October 2, 2015

WAISLAMU WATAKIWA KUZINGATIA MAADILI YAO


Na Steven Augustino,

Tunduru.

BARAZA la Waislamu Tanzania (BAKWATA) wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, limepiga marufuku vitendo vya kufungisha ndoa juu ya dhehebu hilo, pasipo kuzingatia maadili ya dini hiyo.

Sambamba na kutolewa kwa tamko la baraza hilo, pia limeahidi kufuatilia kwa karibu utendaji kazi wa viongozi wake wa dini ambao wamepewa mamlaka ya kufungisha ndoa wilayani humo, na kwa yule atakayekiuka atachukuliwa hatua husika ikiwemo kuzuiwa kufungisha ndoa kwa muumini wa dhehebu hilo.

Tamko hilo lilitolewa na Shekh Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Alhaji Chilakwechi wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu, katika mahojiano maalumu yaliyofanyika ofisini kwake katika Msikiti wa Ijumaa uliopo mjini hapa.


Kwa mujibu wa Shekh Chilakwechi, alieleza kuwa maadili ambayo yamekuwa yakikiukwa na viongozi wenzake wa dini hiyo, wengi wao wamefungisha ndoa ambazo zimehusisha ngoma huku watu wakikesha na muziki mpaka asubuhi jambo ambalo ni kinyume na taratibu za miongozo ya dini hiyo.

Alisema tayari viongozi wenzake wa dini ya kiislamu wilayami humo, tayari wamepewa misingi, taratibu na miongozo kwa kuwataka kutofanya hivyo, ambayo yametolewa na Halmashauri ya baraza hilo baada ya kubaini uwepo wa ukiukwaji mkubwa ambao unafanywa na baadhi ya viongozi wake.

Pamoja na mambo mengine, akizungumzia juu ya suala la uchaguzi mkuu ambao unatarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu, Shekh Chilakwechi aliwataka waumini wa dini ya Kiislaamu kutojiingiza katika malumbano ambayo yanaweza kulisambaratisha taifa letu na kuliweka mahali pabaya.

Hata hivyo alihimiza na kuitaka jamii hapa nchini, kudumisha tunu ya amani na utulivu ambavyo tumerithi toka kwa waasisi wa taifa letu na kuwataka kutambua kuwa baada ya uchaguzi huo, kuna maisha ya Watanzania ambayo yanaendelea kama vile walivyozoea kuishi kila siku.

No comments: