Tuesday, October 13, 2015

CUF TUNDURU YALAANI KUCHANWA MABANGO YA MGOMBEA WAKE

Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHAMA cha Wananchi  (CUF) wilaya ya  Tunduru mkoani Ruvuma, kimelaani vikali kitendo  cha kuchanwa mabango  ya mgombea wake wa udiwani kata ya Mlingoti Mashariki, Mohamed Nyoni.

Kwa mujibu wa taarifa za tukio hilo, zinaeleza kuwa zaidi ya mabango 300 yamechanwa na vijana wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kwamba mabango hayo, yalikuwa yamebandikwa katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo.

Sambamba na kuchanwa kwa mabango hayo, pia taarifa hizo zinasema kuwa watu hao walichana mabango ya mgombea  wao wa ubunge jimbo la Tunduru Kaskazini, anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) Manjolo Kambili.


Madai hayo yalitolewa   na Mkurugenzi wa siasa wa Chama Cha Wananchi (CUF) wilaya  ya  Tunduru, Said Kiosa wakati akiwahutubia wananchi wa kata ya Masonya kijiji cha Nakayaya Mashariki, mjini hapa.

 Alisema kuwa kumekuwa  na hujuma zinazofanyika, kwa lengo  la kuwatishia wananchi wasishiriki mikutano ya kampeni ya Ukawa huku mabango yakichanwa.

Kiosa  aliwataja kwa majina baadhi ya vijana wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi, ambao walichana mabango hayo ni, Mohamed Kumpinduka na Shaibu Mambulu.

Kufuatia hali hiyo, aliutaka uongozi wa Jeshi la Polisi wilayani Tunduru kuwakamata  na kuwachukuria hatua ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Revocatus Malimi amethibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kueleza kuwa Polisi wanaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo, ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.

No comments: