Thursday, October 1, 2015

DED TUNDURU ATAKA VITENDO VYA WAGONJWA KUPIGA WAUGUZI VIDHIBITIWE

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

KUFUATIA kuendelea kuwepo kwa matukio ya wagonjwa wanaolazwa katika Hospitali ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, kuwapiga waganga na wauguzi wa hospitali hiyo Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, ameuagiza uongozi husika kuhakikisha kwamba, vitendo hivyo vinadhibitiwa mara moja.

Sekambo alitoa agizo hilo akiwataka wafanyakazi wa hospitali hiyo, kuzingatia maadili ya kazi zao za kila siku ili waweze kuepukana na migongano isiyokuwa ya lazima kati yao na wagonjwa, wanaokwenda kupatiwa matibabu hospitalini hapo.

“Nimekwisha waagiza viongozi wa hospitali hii, wakae pamoja na kuona wapi kuna tatizo, yawezekana baadhi yao wamekuwa hawatimizi majukumu yao ya kazi ipasavyo ndio maana kumekuwa na matatizo ya kutoelewana, kati ya wafanyakazi wa hospitali na wagonjwa”, alisema Sekambo.


Mkurugenzi huyo alisema kuwa katika hali ya kawaida, haiwezekani mgonjwa achukue hatua ya kumpiga muuguzi wake, bila kuwepo kwa sababu yoyote ile hivyo, lazima kuwepo na jambo ambalo limejitokeza miongoni mwao.

Pamoja na mambo mengine, uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi umebaini kuwa matatizo hayo katika hospitali ya Tunduru yanatokana pia na baadhi ya wafanyakazi wake kutotimiza majukumu ya kazi zao ipasavyo, ndio maana kumekuwa na migongano kati yao na wagonjwa.

Nimezungumza kwa nyakati tofauti na baadhi ya wagonjwa wanaokwenda kupatiwa matibabu katika hospitali hiyo, walidai kuwa jambo hilo limekuwa ni tatizo sugu linaloendelea kuwatesa pale wanapohitaji matibabu hospitalini hapo, na kwamba wanaiomba serikali kuingilia kati ili kuweza kunusuru hali hiyo.


Hata hivyo Mganga mfawidhi wa hospitali ya wilaya ya Tunduru, Dokta Zabron Mmari juu ya madai hayo alithibisha hilo na kusema kuwa hatua zitachukuliwa kwa mganga au muuguzi, atakayekiuka maadili ya kazi ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

No comments: