Tuesday, October 13, 2015

NALICHO: JENGENI UWEZO KWA WATUMISHI WAJIENDELEZE KIMASOMO

Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

SERIKALI wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, imeziagiza idara na taasisi za serikali wilayani humo, kuhakikisha zinawajengea uwezo watumishi wao   kwa kuwapatia nafasi ya kwenda kujiendeleza kimasomo, ili kupunguza tatizo sugu la wataalamu wa kada mbalimbali ikiwa ni lengo la kuongeza ufanisi mahali pa kazi.

Mbali na hilo, wakuu wa idara husika wametakiwa kuwasimamia na kufuatilia kwa karibu watumishi wazembe ambao wanafanya kazi zao kwa mazoea, kitendo ambacho kinasababisha  kutokea malalamiko ya hapa na pale kutoka kwa wananchi.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa wilaya hiyo, Chande Nalicho alipokuwa akizungumza na wakuu wake wa idara katika Halmashauri hiyo na kukemea tabia ya baadhi ya watumishi, kukwamisha kwa makusudi mipango mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na serikali kwa manufaa ya jamii.


Wilaya ya Namtumbo, inakabiliwa  na upungufu mkubwa wa wataalamu katika kada mbalimbali.

“Ninawaagiza wakuu wote wa idara, hakikisheni mnatoa nafasi kwa watumishi wenu kwenda kusoma ili kuwaongezea ujuzi na utaalamu, ambao utasaidia kuleta tija katika wilaya yetu”, alisema Nalicho.

Alisema kuwa, elimu kwa mtumishi wa umma ni jambo muhimu na ndiyo itakayomfanya kujiamini na kutekeleza majukumu yake kikamilifu, badala ya kuendelea kufanya kazi kwa mazoea jambo ambalo linarudisha nyuma maendeleo husika katika jamii.

Katika hatua nyingine, Nalicho amewataka wananchi wa wilaya ya Namtumbo, kuendeleza tunu ya amani iliyopo sasa hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, ikiwa ni lengo la kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuwagawa wananchi na kusababisha nchi, kuingia katika machafuko.


Kadhalika Mkurugenzi huyo amewaomba wazee wa wilaya hiyo, kuwaelekeza vijana wao kuhusu athari na madhara ya migogoro ya kisiasa ambayo tayari imeshaanza kujionesha katika baadhi ya maeneo hapa nchini.

No comments: