Wednesday, February 25, 2015

GAUDENCE KAYOMBO UPEPO WA KISIASA WAENDELEA KUMKALIA VIBAYA MBINGA

Gaudence Kayombo, Mbunge wa Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma.
Na Mwandishi wetu,
Mbinga.

GAUDENCE Kayombo ambaye ni Mbunge wa jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ameendelea kujikuta akiwa katika wakati mgumu kufuatia baadhi ya wapiga kura wake wa jimbo hilo, kuendelea kumlalamikia kwamba tokea achaguliwe katika uchaguzi mkuu uliopita hajawahi kuwatembelea kwenye maeneo yao, jambo ambalo wanakosa imani naye.

Aidha wapiga kura hao walimweleza kuwa, fedha zilizotolewa na shirika la hifadhi ya jamii (NSSF) kwa ajili ya kuwakwamua wakulima wa kahawa ambao wamejiunga kwenye vyama ushirika, hawajanufaika nazo kutokana na kulipwa bei ndogo licha ya fedha hizo kutolewa na shirika hilo kwa riba nafuu.

Walisema wanashangaa kuona malipo waliyolipwa katika msimu wa mavuno ya kahawa mwaka huu shilingi 4,500 ni kidogo, tofauti na makampuni binafsi yamekuwa yakilipa kwa bei nzuri kuanzia shilingi 4,700 hadi 5,000 kwa kilo moja ya kahawa huku yakilipa riba kubwa kwa fedha wanazokopa benki.


Hayo yalijitokeza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jana katika kata ya Nyoni wilayani Mbinga, huku wananchi wa kata hiyo wakizomea pale Kayombo aliposimama na kuanza kuwaeleza kwamba, yeye alikuwa akimtuma katibu wake kuja kuwatembelea, kuzungumza na wananchi kwa lengo la kusikiliza kero mbalimbali na baadaye aweze kuzifanyia kazi.

“Mheshimiwa Mbunge tokea uchaguliwe hatujawahi kukuona katika kata hii, hivi karibuni mmehamasisha wakulima wa kahawa tujiunge na NSSF tutoe michango ili tuweze kupata mikopo yenye riba nafuu kwa sisi wakulima wadogo wadogo ambao tumejiunga katika vyama vya ushirika, lakini tunasikia tu mikopo imetolewa kwa riba nafuu lakini hatunufaiki nayo”, walisema.

Kwa upande wake Mbunge huyo aliposimama na kujibu juu ya hoja hizo walizozitoa wananchi wake, alisema yeye amefanya mambo mengi ya kimaendeleo katika wilaya hiyo huku akimsifia Mkurugenzi mtendaji Hussein Ngaga na Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga kwamba wanasimamia ipasavyo maendeleo ya wanambinga, ambapo wananchi hao ghafla waliendelea kuzomea huku wengine wakisikika na kusema hatukuelewi kwa hayo unayotuambia.

Licha ya Mbunge Kayombo kutumia muda mwingi kujitetea mbele ya wapiga kura wake katika mkutano huo, bado walikuwa hawamwelewi huku wengine wakionekana kutoridhika na majibu aliyokuwa akiyatoa mbele yao. 

Hivi karibuni hata wafanyabiashara wa wilaya ya Mbinga, pia walimlalamikia Mbunge huyo katika kikao chao walichoketi mjini hapa, kwamba tokea achaguliwe pamoja na kumpelekea taarifa wakitaka kuzungumza naye, yeye amekuwa akiwajibu amebanwa na majukumu ya kikazi yupo safarini, hivyo anakosa nafasi ya kukaa pamoja na kuzungumza nao.

No comments: