Thursday, February 12, 2015

TUNDURU WAPITISHA BAJETI, WALIA NA MIRADI YA MAENDELEO



Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

MADIWANI wa Hamashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, wamepitisha bajeti ya halmashauri hiyo, bila mabadiliko na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2015/2016 ya shilingi bilioni 49.4.

 Halmashauri hiyo ilifikia maamuzi hayo katika kikao maalum cha baraza la madiwani ambacho ni cha bajeti, ukumbi wa Klasta ya walimu mlingoti, mjini hapa.

Kwa mujibu wa bajeti hiyo, fedha hizo kati yake shilingi bilioni 37.3 zitatumika kulipa mishahara, bilioni 2.7 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo na bilioni 6.4 ni fedha za miradi ya maendeleo, zote zikiwa zinatokana na ruzuku kutoka serikali kuu pamoja na wadau wa maendeleo.

Aidha halmashauri hiyo inatarajia kukusanya shilingi bilioni 2.6 kutoka katika vyanzo vyake vya ndani.


Akifafanua bajeti hiyo Mratibu wa rasimu ya mpango wa bajeti ya mwaka 2015/2016, afisa mipango wa halmashauri ya wilaya hiyo, Frednand Filimbi alisema kuwa kupitia mpango wa bajeti hiyo, halmashauri yake imepanga kukusanya na  kutumia jumla ya shilingi bilioni 49.438,553,315 katika kipindi cha mwaka huo wa fedha.

Kadhalika aliwahimiza madiwani katika halmashauri yake kuongeza nguvu katika uhamasishaji wa wananchi wao, kujitolea katika utekeleza wa miradi kwenye maeneo yao.

Filimbi aliendelea kufafanua kuwa taarifa za mapitio ya bajeti ya mwaka wa fedha 2014/2015 hadi kufikia mwezi Disemba, halmashauri ilipokea chini ya asilimia 50 ya bajeti yake, hali ambayo alisema kuwa imeathiri utekelezaji wa miradi yao.

Wakichangia kwa nyakati tofati, diwani wa kata ya Mlingoti Magharibi Mchemela Abdalah (CUF), Kitumbi Hamadi wa kata ya Mchesi (CCM) na diwani wa kata ya Marumba Msenga Said (CCM) waliilalamikia serikali kuu, kwamba kitendo cha kutopeleka fedha hizo za ruzuku katika halmashauri yao kwa wakati, kimekuwa chanzo cha kutotekelezeka kwa miradi ya maendeleo ya wananchi katika halmashauri hiyo.

Katika taarifa zao madiwani hao walizungumzia pia, kukwama kwa ujenzi wa miradi ya ofisi za kata ya mlingoti magharibi ambayo ilipangiwa bajeti yake, lakini baada ya kukosekana kwa fedha hizo mradi huo, ulionekana kutotambuliwa na kunyimwa fedha katika bajeti ya mwaka 2014/2015 hali aliyopelekea malalamiko kutoka kwa wananchi.

Madiwani hao walisikitishwa na taarifa za kutokuwepo kwa bajeti ya ujenzi wa madarasa katika shule za msingi, ikiwemo shule ya Msinjili ambayo mwaka 2014 ilipata maafa ya kubomokewa kwa madarasa yake, kutokana na kunyesha mvua ambayo iliambatana na upepo. 

Kufuatia hali hiyo diwani wa kata ya Ligunga (CHADEMA) Kazembe Said, akaja na  hoja ya kuwataka watendaji kutekeleza wajibu wao ipasavyo, ikiwa ni pamoja na kutekeleza ahadi ambazo zimekuwa zikitolewa na viongozi wa serikali.

Kazembe alitolea mfano wa ahadi zilizosahaulika kuwa mwaka 2005 waliokuwa wakuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Kalembo na Monica Mbega waliahidi wananchi wa kijiji cha Mtangashari kuwa, watajengewa zahanati lakini hadi sasa hakuna kilichotekelezwa.

Awali katika ufunguzi wa kikao hicho, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru Faridu Khamisi aliwataka wajumbe wa kikao hicho kuipitia kwa makini bajeti hiyo, na kutoa michango yao kwa uwazi itakayosaidia kuiboresha na kutoa miongozo na maelekezo yaliyozingatiwa, wakati wa kukamilisha maandalizi ya mwisho kabla haijafikishwa katika ngazi za juu kwa ajili ya utekelezaji.

No comments: