Thursday, February 19, 2015

OFISA UTUMISHI MBINGA ANA MATATIZO NI VYEMA HATUA STAHIKI ZICHUKULIWE SASA


Waziri wa nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; Hawa Ghasia.

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

KWA nyakati tofauti baadhi ya watumishi ambao ni Watendaji wa vijiji na kata, wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameendelea kumshutumu Ofisa utumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Emmanuel Kapinga kuwa amekuwa akifanya upendeleo wakati wa upandishaji vyeo kwa watumishi wa kada hizo, jambo ambalo wamedai kuwa kwa namna moja au nyingine, huenda kuna mkono mchafu wa rushwa.

Aidha wameiomba Taasisi ya Kuzuia, Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na vyombo vingine vinavyotetea watumishi kazini, kufanya upembuzi yakinifu ikiwemo kuchunguza mwenendo wa utendaji kazi wa Ofisa huyo, ili kuondoa matatizo yanayoendelea kujitokeza mara kwa mara katika ofisi hiyo na ambayo yanawafanya wakose haki zao za msingi.

Mwandishi wetu, amebaini pia hata utekelezaji wa Waraka wa maendeleo ya utumishi namba moja wa mwaka 2013 ambao unawataka watendaji wakuu katika halmashauri nchini, kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kuwapandisha vyeo watumishi wa kada hizo, amekuwa hatekelezi kwa wakati huku agizo hilo tangu lilipotolewa  na Ofisi ya Rais, chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ndio maana leo linazua malalamiko miongoni mwao.

Pia waraka ulitolewa na Menejimenti ya utumishi wa umma, Februari 27 mwaka 2014 umeagiza na kutaka kutumika kwa miundombinu husika ya utumishi kazini, na kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikijitokeza katika utekelezaji wake hasa kutokana na uhaba wa watumishi wenye sifa zinazotakiwa, katika usimamizi wa rasilimali na miradi ya maendeleo katika ngazi ya kijiji, mtaa na kata.


Aidha umekuwa ukifafanua namna ya upandishaji wa vyeo na ngazi ya mshahara, ambapo utekelezaji wake ulianza mapema Julai Mosi mwaka 2013 huku ukiagiza watendaji wakuu wa mamlaka za serikali za mitaa wanapaswa kushughulikia ajira, maslahi na maendeleo ya watumishi wa kada za watendaji wa vijiji, mitaa na kata waliopo katika mamlaka zao. 

Waraka huo unafuta nyaraka za maendeleo ya watumishi serikali za mitaa namba 29,30 na 31 za mwaka 2003 zilizotolewa na Ofisi ya Rais tume ya utumishi wa serikali za mitaa (TUMITAA) na kwamba watendaji wa vijiji, kata na mitaa waliopo kazini ambao hawana sifa husika wataendelea kubaki katika vyeo walivyonavyo bila kupanda daraja, hadi pale watakapojipatia sifa stahiki.

Hivyo basi, kwa watendaji wa kada hizo wilayani Mbinga, baadhi yao ambao wana sifa ya kupanda daraja na ngazi ya mshahara wamekuwa wakilalamika kwa muda mrefu kwamba hashughulikii ipasavyo masuala yao ya upandishaji wa vyeo, mishahara na hata malipo ya fedha za uhamisho kwa wakati.

Kwa nyakati tofauti walidai kuwa, watakwenda kumshtaki kwenye mamlaka za juu ili waweze kupata haki zao za msingi, ukizingatia kwamba wao ni watumishi wa umma kama alivyo yeye hivyo wanakila sababu kupatiwa haki zao za msingi, kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.

Pamoja na mambo mengine Kapinga, alipotafutwa ili aweze kuzungumzia hilo na kutoa ufafanuzi wa kina juu ya madai hayo, hakuweza kupatikana ofisini kwake na simu yake ilikuwa haipatikani.

No comments: